IMEANDIKWA NA : BEN R. MTOBWA
*********************************************************************************
Simulizi : Salamu Kutoka Kuzimu
Sehemu Ya Kwanza (1)
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
KIFO kaja duniani kwa kazi moja tu. Akikukuta umekwisha... Akikusalimia umekwisha... Hana mdhaha. Lakini sasa huyu anataka watu mashuhuri, watu wakubwa zaidi. Anataka kuifanya Afrika nzima iangue kilio na maombolezo ambayo hayajapata kutokea duniani. Na anataka hilo litokee siku moja, saa moja... "Bendera zote duniani zipepee nusu mlingoti", anasema huku akichekelea. "Sijawahi kushindwa..." Jasho linawatoka watu mashuhuri. Damu inamwagika kama mchezo. Inspekta Kombora machozi yanamtoka. Joram Kiango anabaki kaduwaa.
SURA YA KWANZA
"Bado nasisitiza kuwa tusithubutu wala kujaribu kufanya lolote kabla ya kuhakikisha kuwa Joram Kiango yu marehemu", ilidai sauti moja nzito.
"Naam, lazima afe", sauti nyingine iliunga mkono. "Afe kabla hatujainua mikono kufanya lolote tulilokusudia. Hakuna asiyefahamu jinsi kijana huyu alivyo hatari anusaye shari na kuingilia kati kuharibu harakati zote. Hajasahaulika alivyowakorofisha wale mashujaa waliotaka kuuangusha utawala wa nchi ya Ngoko katika tukio lile lililoitwa Dimbwi la damu. Kadhalika bado hatujasahau alivyosababisha vifo na kuharibu mipango ya majasusi waliotaka kuiharibu nchi hii katika mkasa ambao mtu mmoja aliuandikia kitabu na kuuita Najisikia kuua tena. Kwa kila hali Joram Kiango ni mtu hatari zaidi ya hatari zote zinazoweza kutokea, Hana budi kufa".
Kicheko kikavu kikasikika kidogo, kikafuatwa na sauti iliyokwaruza ikisema.
"Atakufa. Lazima afe. Na atakufa kifo cha kisayansi kabisa. Mpango huu tumeuandaa kwa uangalifu mkubwa, Na watekelezaji wake pia ni watu ambao wamehitimu vizuri katika nyanja zote zinazohusika na kazi hii, Tuondoe shaka kabisa. Mpango huu utafanikiwa kwa asilimia mia".
"Kwa hiyo ndugu Mwemyekiti", ilisema sauti ya mtu wa kwanza. "Niwie radhi kwa kukukata kauli. Ninachokuomba ni kuuahilisha mkutano huu na tusisubutu kukutana tena hadi hapo Joram Kiango atakapokuwa kaburini, Pengine mtaniona mwoga kupindukia, Lakni mimi sipedi kabisa kufanya jambo lolote wakati kijana yule akiwa hai. Mnajua jinsi alivyo na miujiza. Anaweza kuwa hapa akisikiliza mazungumzo yetu, kesho tukajikuta mahakamani bila kutegemea".
Ilizuka minong'ono, sauti mbili tatu zilimuunga mkono msemaji aliyemaliza kusema. Jina la Joram liliamsha hofu katika mioyo yao. Wakatazamana...
Walipenda pia kumwona Mwenyekiti wao uso kwa uso. Kwa bahati mbaya, hawakuweza kuona uso wake isipokuwa kiwiliwili tu, ambacho kilifunikwa kwa mavazi ya thamani kama walivyokuwa wamevaa wao. Mwanga mkali uliotokana na taa ya umeme iliyowekwa kwa namna iliwachoma macho kila walipotamani kumtazama Mwenyekiti usoni. Ni yeye tu aliyekuwa na nafasi nzuri ya kuwatazama wote mmoja baada ya mwinginge kikamilifu na kuwasoma nyuso zao. Wakati wa kumtambua Mwenyekiti ulikuwa bado haujawadia hivyo hawakupaswa kumuona kabisa isipokuwa sauti yake tu.
Mkutano huo ulifanyika katika chumba cha siri, chini ya ardhi katika mojawapo ya majumba ya kifahari yaliyoko Jijini Dar es salaam.
Kila aina ya tahadhari iliwekwa kuhakikisha usalama wa mkutano huu wa awali. Mkutano ambao ulikuwa umeitishwa ghafla, kwa njia za kutatanisha, hata wajumbe hao walijikuta wamefika kwenye mkutano bila kufahamu kilichowaleta hapo.
Mwenyekiti akaufungua mkutano huo kwa maneno machache akisema: "Tunataka kuitetemesha Afrika na kuishangaza dunia. Tunataka kuachia pigo ambalo halitafutika katika historia ya Ulimwengu". Wajumbe wakaelewa kinachoendelea. Ndipo mjume mmoja alipotoa rai ya kumaliza kikao hadi watakaposikia Joram Kiango amekuwa marehemu.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Tahadhari kubwa ilikuwa imechukuliwa wakati wa kuandaa mkutano huo. Wajumbe waliingia kwa siri kubwa wakipita milango tofauti, katika eneo hilo vilitegwa vifaa vya kisasa kwa ajili ya kuhakikisha kila mshiriki wa mkutano huo wa siri anahusika kwa njia moja ama nyingine. Walihakikisha pia hakuna kifaa au chombo chochote cha kunasa sauti ama kusikiliza maongezi hayo ya siri. Vinginevyo chumba hicho kingeweza kutoweka kisayansi kisionekane mlango wowote zaidi ya kuta za kawaida. Zaidi ya yote silaha za kisasa, hewa za sumu, buduki zisizotoa mlio, madawa ya kulevya na mbinu zingine zilikuwa tayari kutumika endapo lolote lingetokea. Kwa bahati mbaya, ni Mwenyekiti peke yake ndiye aliyejua mpango mzima kuhusu mkanda huo.
Kulikuwa na kila sababu ya kuweka tahadhari au uangalifu huo. Watu waliokutana katika mkutano huu hawakuwa watu wenye njaa ya pesa wala kiu ya utajiri. Ni watu mashuhuri walioshiba na kudhamiria kulinda shibe yao. Wote walikuwa na hadhi mitaani, nyadhifa serikalini, na heshima katika chama. Waliokutana hapa wote walikuwa na matarajio ya kuvuna matunda matamu. Matunda ambayo yangetokana na mkutano huo. Hakuna mjumbe aliyependa kukosa utamu wa matunda hayo. Hivyo wote walikuwa na dhamira moja.
"Inaonyesha kuwa Joram ni tishio kwa kila mtu hapa", Sauti nzito ya Mwenyekiti ilisema. "Hilo linanifanya nizidi kuwa na imani juu ya dhamira yenu. Joram anaogopwa kuliko Polisi na jeshi zima la nchi hii, Kwanini? Wanajeshi mko hapa, polisi mko hapa, Chama tawala kiko hapa. Serikali iko hapa. Anayekosekana hapa ni mtu huyo anayejiita Joram Kiango. Mtu mtundu sana, ambaye utundu wake ni madhara kwa watu wenye dhamira maalumu. Hakuna atakayeshuku kuwa kauawa. Daktari atampima na kuona kafa kwa kansa ya moyo. Atauawa kitaalamu na kufa kistaarabu. Msiwe na shaka".
Kimya kifupi kikafuata. Wajumbe wakatazamana usoni. Kimya kilimezwa na sauti ya Mwenyekiti alipoongeza maneno.
"Kwa hiyo, naahirisha kikao hiki kama alivyoshauri mjumbe. Tutakutana tena hapa baada ya wiki mbili, siku na saa kama za leo, kwa njia zetu zile zile, bila kusahau kuwa joram Kiango hatakuwa Joram tena ila hayati Joram Kiango. Na ifahamike kuwa kuitoa nje siri hii ni sawa na kujiwekea saini ya kifo chako mwenyewe".
"Ni kweli Mwenyekiti", sauti mbili tatu za wajumbe wenye hofu, ziliitikia.
Nyumba mbovu zilizojengwa bila utaratibu katika baadhi ya maeneo ya Jiji la Dar es Salaam ambazo huishi kina mama kutoka sehemu mbalimbali nchini ambao humudu kupanga katika nyumba hizi kwa ajili ya makazi na biashara isiyosemekana wala kuitamka. Biashara ambayo ni aibu kubwa kuitaja hadharani, japokuwa inafanyika hadharani bila kificho. Biashara ya kuuza miili kwa pesa chache za matumizi.
Tupo Mburahati, mbele ya moja ya majumba ya aina hii. Kaketi mwanamke ambaye umri wake haujaruhusu kumwita mwanamke. Yu msichana mwenye sura nzuri, mwendo mzuri na kila kitu kizuri, Hata mavazi yake si duni kama wenzake walioketi hatua chache karibu yake, mbele ya milango ya nyumba zao, Kwa jina msichana huyu anaitwa Waridi.
Ni juzi tu Waridi alipotokea hapa Mburahati na kujipatia chumba. Sifa na uzuri wake zilizagaa haraka haraka zikawafikia hata wale ambao si wateja wa biashara hii. Kwamba kaja msichana mzuri.Hakuna aliyetaka kujua katokea wapi, Hakuna aliyetaka kujua kwanini binti mzuri kama huyu aamue kutouthamini uzuri wake ambao ungemfanya aishi vizuri zaidi, akila na kunywa pesa za walionazo. Hakuna aliyejali.
Leo Waridi alikuwa katika hali yake ya kawaida. Hali ya ukimya na majonzi pamoja na kwamba alionekana akiwachekea mara kwa mara wateja wake. Hakuna aliyejua jeraha kubwa lililokuwa moyoni mwake. Jeraha ambalo lilikuwa siri yake na alipenda liendelee kuwa siri. Kutunza siri ni kazi kubwa kama kubeba mzigo mzito usiobanduka kichwani. Mzigo aliobeba kwa dhiki sana. lakini alistahamili kwanki maisha yake yenyewe yalitegemea utunzaji wa siri hii.
Mara akatokea mteja ambaye sura yake, mwendo wake na mavazi yake vilimtofautisha na wateja wa kawaida. Huyu alimtaka Waridi afunge biashara yake siku hiyo ili wafuatane wote nyumbani kwake.
"Haiwezekani. Ninaye bwana wangu ambaye huja kulala hapa".
"Twende kwangu halafu nitakurejesha hapa haraka iwezekanavyo".
"Haiwezekani vilevile".
"Ziko pesa nyingi kwa ajili yako kama utakubali kwenda nyumbani kwangu".
"Nimesema hapana". Ghafla hasira zikampanda Waridi. AKashangaa kwanini kamchukia mtu huyu. "Toka kama hutaki", alifoka na kumwacha mtu huyo kakalia kitanda chake.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Mteja huyu akatabasamu. Kwa waridi lilikuwa tabasamu la kebehi ambalo halikumshitua kuliko alivyotegemea. Swali fupi likaulizwa kwa sauti ndogo. "Huendi na mimi? Hata nikisema kuwa marehemu Bomba ni ndugu yangu pia nafahamu mpaka mahali alikozikwa?".
Hilo lilimshitua kidogo Waridi. Mshituko ulipomtoweka yalifuata machozi mengi yaliyomtoka katika macho yake yaliyoduaa kwa hofu yakimtazama mteja huyo. Mwili wake ulikuwa umemlegea kiasi cha kumfanya ashindwe hata kusimama kikamilifu.
Waridi hakuwa na uwezo wa kufanya lolote. Ndipo mteja huyu alipomsukuma Waridi na kuanguka chali kitandani, akampambua mavazi yote na kumtenda kikatili yote aliyojisikia kumtendea.
Baada ya hapo mteja alimwamru Waridi kufuatana naye. "Tutatoka mara moja. Ukiendelea kukataa nami nitashindwa kutunza siri yako. Twende zetu. Nitakupa kazi ndogo tu, unisaidie. Kuna mtu anahitaji kufa. Utamsaidia wewe. Haitakuwa kazi kubwa kuua mtu wa pili mama. Au vipi? Tofauti pekee ni kwamba yule aliitwa Bomba na huyu anaitwa Joram".
Waridi alimfuata kikondoo.
**********************************
Huyu hakuwa mwingine zaidi ya Jodor Prosper kama alivyojiita katika ule mkutano wa siri uliofanyika usiku wa juzi. Yeye akiwa Mwenyekiti.
Jina hilo lilikuwa moja miongoni mwa majina yake kadha wa kadha ambayo huyatumia wakati tofauti na kwa dhamira tofauti. Kadhalika alikuwa mtu mwenye sura mbalimbali na miondoko aina aina. Kila jamii ilimfahamu Prosper yule yule katika jina na sura tofauti. Vivyo hivyo, tabia zake kubadilika mara kwa mara kama kinyonga anavyojibadili rangi. Katika kundi la wahuni Prosper yu mhuni mkubwa, katika jamii ya waungwana yu muungwana halisi, katika familia ya masikini Prosper alikuwa mmoja wao, na miongoni mwa matajiri yeye ni kama wao.
Huyo ndiye Prosper. Mswahili aliyezaliwa mahali fulani katika Pwani ya Bahari ya Hindi. Akiwa na miaka kumi na miwili, alitoweka numbani kwao kwa kudandia meli moja iliyotia nanga katika Bandari ya Tanga.
Meli hiyo iliyokuwa na mabaharia katili kupita kiasi. Walimpokea Prosper kwa ukatili usiosemekana. walimtendea mengi maovu, akitukanwa na kusimangwa. Aliishi kwa taabu mno, akiyastahamili yote hayo, mwishowe, akawa mnyama kama mabaharia wale.
Alisuguliwa akasugulika, akageuka kuwa Baharia binadamu mwenye moyo wa mnyama. Akamchukia kila mtu na hata kuichukia nafsi yake mwenyewe. Wakati wote Prosper alitawaliwa na fikra potofu. Alitamani kutenda jambo ambalo lingeiumiza jamii. Kwa bahati mbaya, hakuwa mwana sayansi mwenye vipaji vya ugunduzi, ugunduzi ambao ungemwezesha kuiteketeza jamii. Angekuwa na uwezo wa kujitengenezea bomu la nuklia angeifanya dunia itoweke katika uso wa ulimwengu.
Kwa kuwa, hayo yalikuwa mbali na uwezo wake, lakini alifanya ukatili mdogo tu. Hakuona shida kumtosa baharini mtu yeyote aliyebainika kudandia meli kama alivyofanya yeye alipokuwa mtoto. Wala, kwake haikuwa dhambi kufanya mapenzi na mwanamke na kisha kukata koo la mwanamke huyo asubuhi.
Pamoja na ukatili huu kuufanya kwa siri, lakini sifa zake ziliyafikia masikio mbalimbali. Mmoja kati ya watu waliovutiwa na unyama wa Prosper aliona fahari kukutana nae katika meli hiyo kwa siri. Wakaiacha meli hiyo. Safari yao ikaishia katika chuo kimoja kilichofichika kikiwa na watu wachache wenye moyo kwama wa Prosper. Kilikuwa chuo cha ujasusi kilichokuwa chini ya nchi kadhaa kubwa na tajiri. Kilifundisha mbinu kadha wa kadha kuhujumu siasa, uchumi na msimamo wa nchi kongwe na changa ambazo hazikuwa tayari kulegeza misimamo yao na zile zenye msimamo mkali.
Prosper alipohitimu tayari alikuwa hodari wa yote, kuandaa mauaji, kusababisha mapinduzi, kudhorotesha uchumi. Alikuwa mtu aliyeipenda sana kazi yake, na alifanya mengi yaliyowafurahisha na kuwatisha viongozi wake. Aliweza kusafiri hadi Afrika Kusini ambako alijitangaza kama mpigania uhuru na aliaminika na kushirikishwa katika harakati za ukombozi. Lakini aliweza kutoroka na siri zote huku akiwa tayari ameua na kuwaacha wapigania uhuru wakiuana wenyewe kwa wenyewe. Mtindo huo ameutumia sehemu mbalimbali duniani. Ingawa waliohujumiwa walimhisi baada ya kuondoka, lakini kwa jinsi alivyokuwa akiwaendea katika sura tofauti, na majina bandia, hakuna aliyeweza kumweka katika kumbukumbu.
Mfano ni leo alipokuwa akitoka na msichana huyu aliyechanganyikiwa; Waridi. Wajumbe wote wa mkutano ule ambao walibahatisha kuuona uso wake wasingeweza kumfikiria kuwa ndiye mtu yule yule waliyekuwa naye mkutanoni kwa jinsi alivyobadilika. Hata mwendo wake ulikuwa tofauti. Leo alitembea huku akichechemea kidogo.
Gari dogo aina ya Toyota lilikuwa likiwasubiri mara tu walipoifikia barabara.
"Ingia ndani ya gari", Prosper aliamuru.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Samahani..., samahani kaka, tu... tunaelekea wapi?", Waridi alifanikiwa kuupata ulimi wake ambao alihisi ulikuwa mzito kutokana na hofu.
Prosper akaukunja uso wake huku akisema, "Sitaki maswali", akapita upande wa dereva na kumfungulia mlango Waridi. Alipoingia ndani ya gari na kuketi, gari likatiwa moto na kuteleza juu ya barabara, likijitahidi kukwepa mashimo. Walipoifikia barabara ya Morogoro, gari hilo liliekezwa katikati ya jiji. Wakaiacha Magomeni, wakaingia Upanga, wakipita hapa na pele hata waridi asijue kama walikuwa wapi,
Gari lilisimama mbele ya jumba moja kubwa sehemu ambayo hisia zilimwambia Waridi kuwa ni katikati ya Jiji. Prosper alitelemka na kumwagiza Waridi amfuate. Walipokaribia mlango mmoja kati ya milango kadhaa ya jumba hilo, Prosper alimnong'oneza Waridi akisema; "Unasikia? sitiki vurugu la aina yoyote hapa ndani. Uwe binti mtulivu kama ulivyo sasa. Utafaidika na kutoka salama. Vinginevyo..." akaiacha sentesi hiyo ikielea na kuanza kushugulikia funguo.
Walipoanza kuingia, mlango wa pili ulifunguka na uso wa mzee wa Kihindi kujitokeza ukichungulia. "Aha... ni bwana Chain siyo? Karibu sana".
"Shukrani", Prosper alijibu.
"Naona leo uko na mama, au siyo?, Mhindi huyo aliendelea akitabasamu. "Shauri kazi ya vitabu iko chosa kidogo. Lazima starehe na dada kidogo".
Prosper naye akajitia kucheka, "Eh, ndiyo. Lakini huyu ni sekretary wa kampuni yetu. Yeye amekuja kuchukua maandishi fulani kwa ajili ya kuchapishwa kwenye mashine wakati nitakapokuwa safarini".
"Ah", Mhindi alijibu huku akimtazama Waridi kwa tamaa ya wazi. Hili lilikuwa moja kati ya majumba ambayo Prosper alikuwa amepangisha vyumba ambavyo aliviyumia kwa shughuli zake. Hapa, mbali na kufahamika kwa jina la Chain Kimara, pia walimtambua kama msomi ambaye alikuwa akiutumia muda wake mwingi kufanya utafiti wa mambo kadha wa kadha ambayo alikuwa akiyaandikia kitabu. Hivyo, muda wote ambao Prosper alijificha chumbani akifanya shughuli zake za siri, wao waliamini kuwa alikuwa akiendelea na mipango ya kuhakikisha kitabu chake kinatoka. Akiwa hapa, hata sura yake ilionekana kama ya Profesa asiyependa kuuchezea muda wake kama ilivyokuwa tabia yake ya kisomi na kistaarabu.
Huko ndani picha ilikuwa hiyo hiyo, Waridi alilakiwa na chumba kikubwa kilichojaa vitabu vya kila aina , vilivyopangwa kistaarabu katika dawati maalumu. Katikati ya chumba hiki kulikuwa na meza kubwa yenye dalili zote za mashughuliko. Chumba cha pili kilikuwa na kitanda kipana, friji, radio na mahitaji yote ya chumba cha malazi. Ni katika chumba hicho alikokaribishwa Waridi.
Akajibwatika juu ya kochi lililomwelekea Prosper, aliyeketi juu ya kitanda.
"Nimekuita hapa ili nikutume kuua mtu", Prosper alimweleza Waridi. Dakika ishirini zijazo nataka mtu huyo awe safarini akielekea kuzimu. Sasa hivi yuko katika baa moja hapa mjini akinywa pombe. Hiyo iwe pombe yake ya mwisho", Prosper alisita akamtazama Waridi. "Utanisaidia kuifanya kazi hiyo bi mdogo", akaongeza kwa sauti ya unyenyekevu.
"Siwezi kuua..." Waridi aligugumia.
Prosper alikunja uso akamwangalia Waridi kwa hasira huku akisema. "Sina haja ya kukukumbusha mara kwa mara kuwa najua yote yaliyompata marehemu Bomba. Naweza kutoa siri hiyo wakati wowote nawe ukajikuta ukining'inia juu ya kitanzi. Nitakufanyia hisani ya kuficha habari hiyo iwapo tu nawe utanisaidia kumtoa duniani mtu huyu. Tumeelewana?",
Waridi hakujua ajibu nini. Kwa kila hali. alimwona mzee huyu kampatia na kamweka mahali panapomstahili. Hofu yake kubwa haikuwa kitanzu tu bali ilimuumiza kutajiwa mara kwa mara jina hilo la Bomba. Ilimuumiza sana kukumbuka kifo cha mtu huyo kilivyotokea na jinsi alivyotoa macho wajati anakata roho. Ilimuumiza zaidi Waridi kukumbuka kuwa dhambi hiyo ya kuua alikuwa ameifanya bure kabisa.
Ni miezi kadhaa tu iliyopita. Wakati huo Waridi alikuwa Waridi wa ukweli. Ua la uhakika ambalo kila nyuki alilitamani, kila kipepeo alilimezea mate. Lakini si wote waliolifikia. Na wachache waliofaulu kuligusa, hawakuwa vipepeo wala nyuki wa kawaida. Walikuwa zaidi.
Uzuri wa msichana huyu ulianza kujitokeza tangu alipokuwa kinda. Alipofikia umri wa miaka mwili tu, kila mtu alibaini kuwa mtoto huyu alikuwa hazina ya uzuri. Alipofika miaka sita watu walianza kunong'ona. Alipohitimu miaka kumi, wanaume wasiokuwa na staha, walianza kumnyatia. Miaka kumi na miwili Waridi alikuwa tayari akiwa kama malkia wa nyuki na kama nilivyosema awali; kwa vipepeo.
Pengine uzuri wake huo ulitokana na ule mchanganyiko maalumu katika umbo lake. Mchanganyiko wa damu za watu weusi, Wahindi, waarabu na Wazungu ambao walishiriki kumtengeneza. Kwani mama yake pia alikuwa mtu wa nipe nikupe. Alifanya biashara yake katika mji wa Mwanza, katika mojawapo ya vibana vibovu, akimkaribisha yeyote mwenye 'chochote'. Mama huyu hakumfahamu kabisa mtu maalumu aliyeshirikiana naye kumpata Waridi binti yake wa pekee. Alichofahamu ni kuwa, kumpata binti mzuri ambaye watu walianza kumwita Waridi, hata jina lake la awali likasahaulika.
Kwa Waridi hakujua kama alikuwa mzuri kupidukia, lakini alishangaa kuwaona watu wazima kwa vijana wakimfuata na kumtaka kitu ambacho hakukifahamu maana ama umuhimu wake. Kitu kile ambacho alimwona mama yake akikifanya mara kwa mara kitandani.
Kisha akafahamu. Ilikuwa baada ya kukamatwa kwa nguvu na mzee mmoja aliyemtupa sakafuni, akamvua nguo na kumwingilia miguuni kwa namna ambayo ilimtia Waridi maumivu makali yaliyoambatana na faraja.
Waridi akayafahamu hayo, akaifahamu thamani ya uzuri wake, akaanza kuingiwa na kiburi. Akajidekeza na kutupilia mbali masomo. Huyo akamtoroka mama yake na kuingia mjini Tabora,ambapo aliishi kwa faraja kubwa. Daima wanaume walikuwa tayari kumhudumia kwa maneno matamu, malezi, mavazi huku akipewa fedha za kutosha.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Lakini Waridi hakutosheka. Daima alidai hiki na kile kwa wanaome ambao kila mmoja alijitahidi kutoa alichonacho. Lakini baada ya kupata walichohitaji wakamwepuka. Hivyo akauona mji wa Tabora haufai. Akasogea hadi Dodoma ambapo pia hakukaa sana, akapanda hadi Arusha. Mji huo ulipomchoka, akapaa na kushuka Jijini Dar es Salaam.
Ni hapo alipokutana na Bomba Kimara. Kijana huyu mwenye asili ya Kiarabu mtu ambaye Maua alimhitaji. Siku zote alionekana 'kajaa', Fedha kwa Bomba hazikuwa na tatizo. Wala hakuna uchungu kuzitumia. Kadhalika, fedha zake hazikuwa mfukoni kama wanaume wengine. Zake zilitoka katika soksi. Kitita cha elfu kumi kumi kikiwa kimefungwa kwa mpira kingewezaje kukaa mfukoni? Walizitumia fedha hizo na Waridi wakishirikiana kuhama baa moja kwenda nyingine, madansa, sinema, mahoteli na kila aina ya starehe.
Walikuwa wakiishi Magomeni Mikumi katika nyumba za msajili wa majumba ambayo Bomba alikuwa amekodi. Ni mara chache sana nyumba hii ilipowaona wapangaji wake, kwani mara nyingi walikuwa kama si Kunduchi Beach, basi wako Kilimanjaro Hoteli au Mbowe Hoteli na sehemu nyingine za starehe wakitumia.
Halafu ikafika ile siku ambayo Bomba alirudi nyumbani mapema kutoka kule alikokuwa akienda mara kwa mara na kurudi na pesa. Safari hii alirudi na mfuko wa ngozi ambao aliutua juu ya kitanda. Alionekana mtu mwenye wasiwasi mwingi kinyume na tabia yake. Hakujua kwa Waridi alikuwa chumbani humo akimtazama.
"Vipi mwenzangu?" Sauti ya Waridi ilimzindua. Akamgeukia akijaribu kutabasamu lakini tabasamu lilikataa.
"Waridi, kwenu ni wapi?" Bomba alihoji ghafla.
Swali hili lilimshangaza sana Waridi. Muda wote walioishi pamoja hawakuwahi kuulizana maswali ya aina hiyo.
'Kwanini?" Bomba akaendelea. "Nataka urudi kwenu. Mimi naona maisha hayaniendei vizuri", Bomba akaeleza. Baada ya kunyamaza kwa sekunde kadhaa, akasema.
"Waridi, ni hadithi ndefu ninayo. Hadithi ambayo haifai kulifikia sikio lisilohusika. Ninachoomba ni wewe kwenda zako kesho. Kama hutaki kwenda nyumbani kwenu, rudi kwenye baa niliyokukuta. Naamini ukirudi pale baa haitapita dakika tano kabla hujaokotwa na mwanaume mwingine".
"Kuokotwa?" Maua alijiuliza kwa hasira. Ghafla alijikuta kamchukulia Bomba kama mtu shetani. Hata sura yake sasa aliiona mbaya kama dhambi. Machozi yalimtoka na kuteleza juu ya mashavu yake. Akainuka na kutoka nje kimya.
Waridi alirudi ndani baada ya kumsikia Bomba akioga bafuni. Akafanya haraka kuuendelea ule mfuko ambao aliufunua. Macho yake yalikutana na furushi kubwa la noti ambalo hakuwahi kuliona katika maisha yake. Kwa kukadilia zilikuwa pesa nyingi. Kando ya pesa hizo, ililala bastola kubwa na tiketi moja ya ndege. Tiketi hiyo ilionyesha jina la Bomba kuelekea Nairobi.
Wazo likamjia Waridi. Bomba alikusudia kumtupa baada ya kupata pesa nyingi kama hizo ili aende zake Nairobi akatumie peke yake! Waridi akajishauri kuchota pesa kidogo afiche. Akasita. Alizihitaji zote. Akaamua kuzipata. Akazirudisha kama zilivyokuwa akatoka zake nje.
Usiku huo, Waridi alikuwa wa kwanza kulala. Alijitia kulia pole pole kwa namna iliyokusudiwa kumfanya Bomba aamini kuwa Waridi alimpenda kwa dhati. Ukweli ni kwamba katika maisha yake Waridi hakuwahi kumpenda mwanaume. Alipeda pesa. Mwanaume alimhitaji kwa ajili ya faraja ya mwili tu.
Bomba alikuwa amelala kando yake, alipoanza kukoroma, Waridi aliamka taratibu, akanyata hadi uani ambako alilibeba kwa taabu jiwe kubwa alilokuwa ameliandaa mchana. Akaingia nalo hadi chumbani ambako Bomba alikuwa akiendelea kukoroma. Akakilenga barabara kichwa chake na kuliachia jiwe lile.
Bamba alikurupuka kutoka usingizini na kupaa juu, alipotua kitandani. Alitoa mlio wa maumivu kwa sauti ndogo nyembamba ambayo ilimwingia Waridi rohoni na kumtia ganzi. Kichwa cha Bomba kilikuwa kimefumuka. Ubongo uliochanganyika na damu ulikuwa ukivuja kitandani na kuchafua mashuka. Lakini bado aliendelea kutapatapa huku na kule, akisema hili na lile, maneno ambayo Waridi hakuweza kuyaelewa. Ni macho yake ambayo yaliweza kumtisha Waridi zaidi... Macho ya Bomba yalikuwa yakimtazama kwa namna ya huruma na kutoamini alichokifanya.
Waridi hakuweza kustahamili. Akapiga kelele kwa hofu akakimbia nje ya chumba hiki ambako aliketi chini akitetemeka. Baada ya muda, alirudi ndani ambako alimkuta Bomba tayari amekuwa marehemu; domo wazi, ulimi ukiwa umesahaulikwa nje, upande mmoja ilikuwa kama picha ya kusikitisha inayotisha mno. Waridi akaona shida kuistahamili. Akajikaza kiume kwa kumfungafunga marehemu Bomba kwa blanketi kubwa kisha akajaribu kumuinua ili amtoe nje. Hakufaulu. Akamvuta hadi uwanni. Huko akajitahidi na kuifikisha mati chooni ambako kulikuwa na tundu kubwa lililofunikwa na bati. Akalifunua bati hilo, na kumtumbukiza marehemu Bomba. Kisha akalifunika kama lilivyokuwa awali.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Wazo lake sasa lilikuwa moja tu; kuzihesabu pesa zake kikamilifu, Lakini mwujiza ulikuwa ukimsubiri. Mfuko wa pesa ulikuwa umetoweka. Haukuwepo tena juu ya kabati, ambapo aliuona kwa mara ya mwisho kabla ya kuutoa mzoga wa aliyekuwa mpenzi wake Bomba ndani. "Uko wapi?", Waridi alijiuliza huku akiutafuta mfuko huo kila kona ya nyumba bila mafanikio. Akabaki ameduwaa.
Mapambazuko yalimkuta bado kaduwaa katikati ya chumba, macho yakilitazama kabati kwa mshangao kana kwamba limeumeza mfuko huo wenye pesa. Waridi hakujua afuate lipi aache lipi.
Mara akajikuta akitoka nje ya nyumba hiyo. Alitembea kwa mkiguu hajui aendako. Baada ya kutwa nzima ya mzunguko usio na dhamira maalumu, Alielekea Mburahati ambako hakukawia kupata rafiki aliyemkarimu kwa kumsaidia kupata chumba cha muda. Baadae, Waridi alipata chumba chake. Siku zote moyo wake uliteswa na huzuni akikukmbuka kumwaga damu ya mtu asiyekuwa na hatia, hofu kwa kudhani kuwa wakati wowote polisi wangeweza kutokea kwa ajili ya kumchukua, na zaidi, maumivu makali moyoi kwa kuhisi ile sauti ya Bomba alipolia kwa uchungu na picha ya macho yake yalivyokuwa yakisihi.
Waridi hakuwa na la kufanya. Maisha yalimwendea vyema katika mazingira yake mapya, wateja wakimiminika kwa wingi hadi leo alipotokea mtu huyu wa ajabu ajabu ambaye anafahamu kila kitu kuhusu mkasa juu ya kifo cha Bomba.
"Siwezi... Siwezi kuua tena...?"Waridi alisema huku akibubujikwa na machozi.
"Huna ujanja, lazima utaua".
"Utaua?", Prosper alifoka kwa nguvu akiachia kofi kali ambalo lilimwingia Waridi kama aliyepigwa na kipande cha ubao. Akiwa msichana asiyezoea kupokea vipigo kutoka kwa wanaume, kofi hili lilimshangaza zaidi zaidi ya jinsi lilivyomwumiza. Lakini mshangao wake ulikoma pindi Prosper alipoongeza vipigo vingine vikali zaidi ambavyo vilimfanya Waridi ajikute akighalaghala chini damu zikimvuja hovyo kutoka usoni, puani na mdomoni.
Prosper akaangua kicheko, "Well", akasema, nilikuwa sikupigi ila tu ilikuwa kukuandaa katika hali ambayo itakufanya umpate Joram Kiango kwa urahisi. Yeye ni mtu anayevutiwa sana na mambo ya damu. Hivyo atakapokuona atajileta mwenyewe kwako. Utakachofanya wewe ni kuhakikisha umempata dawa ambayo nitakupatia, Baada ya muda mfupi atakuwa marehemu. Itaonekana kafa kwa magonjwa ya kawaida tu. Hakuna atakayefikiria kama wewe na mimi tunahusika na kifo chake",
Prosper alinyamaza kidogo akimwangalia waridi kuona kama maelezo yake yalikuwa yakimwingia, alipoona maneno yake yameanza kumwingia Waridi. Akaendelea. "Unaona iivyo kazi rahisi. Ni kazi ndogo tu. Inatofati sana na ile kubwa uliyofanya wakati ukimuua marehemu Bomba".
Moyoni Prosper aliwaza; Waridi angejisikiaje kufahamu kuwa yeye Prosper muda wote ule alikuwa nje akisubiri fursa ya kumuua Bomba! Kwani, Bomba ambaye alikuwa mmoja wa magaidi wake, alikuwa ameshindwa kutimiza kazi fulani aliyopewa. Badala yake alipanga kutoroka na pesa ambazo alipewa kwa ajili ya shughuli maalumu. Ndipo ilipodi Bomba auawe usiku ule. Ni Prosper pia aliyepeya hadi ndani na kuzichukua pesa zile baada ya kuona kazi aliyokusudia kuifanya ilikuwa imefanywa na Waridi.
Prosper aliitazama tena saa yake. "Bado dakika tano Waridi", Prosper alimwita Waridi, "Simama haraka ujiandae".
Kiasi fulani Waridi alikuwa hoi, hivyo alishindwa hata kusimama, lakini Prosper akamsaidia na kumwongoza nje ambako walipanda gari. Humo garini, Prosper alitoa amri nyingine ambayo Waridi hakuitegemea.
"Vua nguo zako zote".
Waridi aliduwaa na akasaidiwa kuzivua. Prosper hakusita kuzitatua.
"Nataka ufanye kazi nzuri tafadhali. Shika hii... Kamata na hii... Ni kazi ndogo sana... Kesho Joram Kiango atakuwa marehemu"?.
Baa hii ilikuwa imejaa watu wa kila aina; waliokuwa wakinywa na kustarehe kwa namna mbalimbali. Miongoni mwa watu hawa, alikuwemo Joram Kiango.
Yeye alitulia pale kaunta, juu ya stuli ndefu, pombe ikiwa wazi mbele yake, sigara ikiteketea mdomoni mwake. Kama ni furaha, yake ilikuwa tofauti na walevi ama wanywaji wengine. Hakusinzia hovyo wala kucheka pasipo sababu. Ukimya wake ulimfanya hata msichana wake Neema, ambaye alikuwa kando akinywa soda, amgeukie na kusema polepole.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Tatizo lako ndio hilo, Joram. Uwapo huru unashindwa kuutumia uhuru wako. Tazama usivyo na raha. Mtu yeyote anayekufahamu akitokea hapa atadhani uko kizimbani ukisubiri hukumu ya kifo, badala ya kustarehe. Kwa nini?".
Joram aligeuka kumtazama huku akimtengenezea tabasamu jepesi. Kama kawaida, macho yake yaliona kile ambacho yamezoea kuona katika umbo la msichana huyo. Umbo lenye urefu wa kadri, unene wa kadri na sura ambayo ilioana vizuri na umbo hilo. Sura ambayo ilisisimua moyo wa kila mwanaume aliyepata kumtupia macho Neema. Kadhalika, mavazi ya Neema yalikuwa ya kupendeza na yaliliafiki umbo lake. Lilikuwa gauni la kitambaa chepesi ambacho ni dhahiri kilitokea nje ya Afrika Mashariki. Si hayo tu yaliyomfanya Joram ampende Neema na kumthamini binti huyo. Macho ya mwanadada huyu yalikuwa na uzuri wa pekee, uzuri wa kubembelezabembeleza, uzuri wa kishujaa. Yalikuwa na nuru. Si nuru wa "mapenzi" bali nuru ya ujasiri.
Ujasiri huo ndio aliouhusudu Joram. Na ni kwa ajili ya kuuthamini ndipo mara kwa mara akawa akimshinda nguvu shetani wake ambaye alikuwa akitamani kumtia mweleka kwa kumnong'oneza akisema: "Sikia Joram Neema ni binti mzuri sana... na anakupenda sana... Kwa nini usisahau walao kwa siku moja awe mwenzi wako kikazi akastarehe naye kitandani?... Hujui... Utakuwa usiku mzuri kuliko usiku wowote mwingine..." Hayo Joram aliyapuuza na kuendelea kumwona Neema kama mpenzi wake wa dhati.
Mawazo hayo yalimjia tena Joram. Wakati huo, badala ya kumjibu Neema swali lake, alitabasamu tena, kisha akavuta sigara kwa utulivu. Tayari kusahau yote.
"Tazama!" Neema alilalamika. "Bado hata unashindwa hata kunijibu! Wamekuloga nini kaka yangu? Kwa kweli sijaiona siku yoyote ambayo uko kwenye starehe isipokuwa hapo tu unapokuwa vitani ukipambana na mikasa ya kutatanisha huku maisha yako yakiwa hatarini. Sijasahau niliposoma katika gazeti la Kiongozi jinsi ulivyokuwa ukicheka mbele ya bastola ya kumwuaji yule hatari katika tukio lililoitwa Lazima Ufe... kule Arusha".
Tabasamu la Joram likageuka kicheko, "Mimi nilidhani kwamba wewe unanielewa vizuri zaidi mpenzi", alisema. "Tatizo langu ni watu kutokunielewa. Hapa nilipo, kimya kama nilivyo, nina furaha na nimestarehe kabisa. Lakini watu watadhani sina raha. Niwapo mbele ya bastola huwa sicheki bali nimechukia sana. Tabasamu langu huwa ni moja ya silaha zangu kwa ajili ya kumlegeza adui. Kwa kweli silaha hiyo naipenda zaidi ya bastola. Kwani humfanya adui ashindwe kuitumia bastola yake.
"Huwa huna hofu?".
"Sijui hofu ni kitu cha aina gani kwa kweli. Labda itabidi nimpate daktari mzuri anipime na kuona kama ninazo chembechembe za kitu hicho kinachoitwa hofu katika moyo wangu. Nadhani hili kwangu ni lazima..."
Neema akaangua kicheko. "U kiumbe wa ajabu sana Joram. Unaona sasa ulivyochangamka baada ya kuanza mazungumzo ya vifo na mauaji? Nadhani kifo chako kitakuwa cha kusikitisha sana".
"Ni afadhali kuliko kufia juu ya kitanda Muhimbili, tena baada ya kuugua miezi kadha wa kadha".
Wakati mazungumzo hayo yakiendelea, macho ya Joram yakauacha uso wa Neema na kumtazama mtu ambaye alikuwa ameingia ghafla katika baa hiyo. Pamoja na kuingia kama watu wengine, akiwa katika mavazi ya kawaida, suti nyeusi, macho yake yalimvutia Joram. Macho yake yakaonyesha dalili ya wasiwasi na tahayari. Joram hakuona kama wasiwasi huo ulikuwa wa kuwahi pombe. Hilo alilidhihilisha kutokana na macho hayo yalivyotembea huku na huko ndani ya baa. Yalipokutana na macho ya Joram, yalizidi kupatwa na hofu kubwa. Kisha mtu huyo akageuka ba kutoka nje. Mara kilio kikali kikasikika kutoka nje. Ilikuwa sauti ya msichana, akilia kwa uchungu.
"Mwanamke malaya, anapokula pesa za watu wahuni hupelekwa gizani ambako hufanyiwa unyama", lilikuwa jibu la Joram.
"Umejuaje kuwa ni mwanamke malaya Joram?", Neema alihoji. Wakati huo watu walikuwa wakitoka ndani ya baa kwenda nje kutazama. "Anaweza kuwa mke wa mtu aliyekamatwa na kuletwa huku kwa ajili ya kutendewa unyama, twende tukaone".
"Hatuna muda huo..."
"Twende Joram". Wakati huo Neema alikuwa wima akimvuta Joram. "Twende tafadhali..." Ikamlazimu Joram kukubali. Umati wa watu ulikuwa ukielekea nyuma ya baa, sehemu ambayo ilikuwa na kivuli chenye giza kilichotokana na msitu wa maua yaliyoizunguka baa hiyo.
Japo ndipo sauti ya msichana huyo ilisikika akilia.
Alikuwa kalala chali, nusu uchi, vazi lake pekee ilikuwa kipande kidogo cha kanga ambacho kilifunika sehemu ya kati na kuruhusu sehemu kubwa isiyostahili kuonekana hovyo, itazamwe na watazamaji.
"Nakufa jamani, nakufa..." binti huyo aliendelea kulia huku akitupa miguu huku na kule.
Mtu mmoja alikuwa na tochi. Akamulika. Mwanga wake ulinisa kitu cha kutisha zaidi. Damu. Damu nzito ilikuwa imetapakaa kando na juu ya mwili wa msichana huyo. Mara kitu cha kutisha zaidi kikaonekana. Kisu! Kisu kirefu chenye damu. Kilikuwa kando ya mwili wa msichana huyo.
"Kisu jamani", mtu mmoja alilalamika.
"Nakufa... nisaidieni..." msichana huyu aliendelea kulalamika.
Kiasi Joram akaanza kuvutiwa. Hata hivyo Joram hakuvutiwa na kisu wala damu tu. Alikuwa akiutazama uso wa msichana huyo. Aliyaona macho yake. Alikuwa msichana mzuri sana isipokuwa macho yake tu. Yalikuwa macho yale yale aliyoyategemea kitambo. Macho ya msichana mlevi na malaya ambaye amekula vya watu na sasa vinamtokea puani. Hivyo aliushika mkono wa Neema na kumwambia. "Inatosha twende zetu".
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Joram! Tumwache msichana huyu katika hali hii kweli?" Neema alilalamika.
"Ni kazi ya polisi. Haonyeshi kama atakufa".
"Nakufa", binti huyo aliendelea kulia. "Upo hapo Joram? Tafadhali nisaidie. Inama usnishike japo mkono. Naogopa wataniua. Tafadhali Joram".
Kutajwa kwa jina la Joram kilisababisha watu waliokuwa hapo wamsahau msichana huyo mahututi, wakagauka kumtazama Joram, kijana mzuri wa sura, mrefu, nadhifu kwa mwili na mavazi, alionekana mpole tofauti na ilivyofikiriwa. "Kumbe huyu ndiye Joram Kiango!", walinongona watazamaji. Mara kadha wamesoma habari zake magazetini na kutegemewa kuwa labda lilikuwa pandikizi la mwanaume linaloweza kuwatisha majambazi. Kumbe.
"Nisaidie Joram..." msichana akaendelea kulalamika.
Joram ni mtu anayechukia kutazamwatazamwa na kushangiliwa, basi aliondoka polepole huku akifuatwa na Neema. Alipofika ndani akakiendea kibanda cha simu na kuzungusha 999. Sauti ilipomjibu alisema. "Hapa ni Forest of Flowers Bar... ndiyo Kinondoni. Njooni kuna mtu wenu anavuja damu..."
Polisi waliotummwa kuja kumchukuwa 'majeruhi' huyo walikuwa vijana wawili wenye imani moja dhidi ya wanawake malaya; kwamba malaya ni mwizi wa mchana. Hivyo, inapotokea akapigwa hata kuuawa ni haki yake kabisa.
Wakiwa na imani hiyo, polisi hao walimzoa Waridi bila huruma wala kujali malalamiko yake. Kama kuna jambo liliwasikitisha ni kule kuona kuwa kipigo alichopata hakikumsitahili kabisa. Majeraha machache yaliyokuwa usoni mwake na damu kidogo iliyokuwa ikivuja polisi hawa hawakuona kama ni adhabu iliyomtosha malaya kama huyu. Kama kuna jambo liliwashangaza polisi hawa, ni kuona kuwa kisu hicho kikali kilicholala kando yake hakikutimiza wajibu. Yawezekana washambuliaji wake walikuwa waoga, au hawakudhamilia lingine zaidi ya kumtisha tu.
Gari lilipoanza kuondoka, polisi hawakuchelewa kumtupia maswali kadha wa kadha, maswali ambayo hawakujali kusikiliza majibu yake. Na kwanini wapoteze muda kusikiliza uongo ulioandaliwa kitambo? Mmoja wa vijana hawa akajikuta kavutiwa na uzuri wa Waridi. Kwa kisingizio cha kumfuta damu, akanyoosha mkono wake na kumgusa titi lililokuwa wazi likiwatazama kama linawadhihaki. Mkono ukanogewa na kutelemshwa hadi kwenye paja lake jekundu lililonona. Mkono huo ukaanza ziara nyingine ya kupanda juu. Ulipoelekea kuvuka mipaka, Waridi akashindwa kustahamii zaidi. Akainua mkono wake na kuunasa mkono wa askari huyo na kuutoa juu ya paja lake. Baada ya kitendo hicho, Ndipo alipotanabahi kuwa kamgusa askari huyo kwa mkono ulioandaliwa maalumu
kwa ajili ya mtu mmoja tu, Joram Kiango. Waridi alijua kitakachomtokea askari huyo. Mara akaangua kilio kwa sauti kubwa. Kilio ambacho kiliwashagaza askari hao.
Walifanikiwa kumfikisha katika hospitali ya Mwananyamala ambapo alipokelewa na wauguzi wa zamu. Askari hao wakaaga na kuahidi kurudi hospitalini hapo kesho yake ili kuanza upelelezi wao.
Waridi aliwaomba wauguzi kumpeleka moja kwa moja bafuni. Huko alitupa dawa zote alizohifadhi mkononi, akanawa vizuri kwa dawa kama alivyoelekezwa na Proper. Ndipo aliporudi kwa wauguzi ambao hawakuonyesha nia ya kumhudumia kutokana na hali yake alikuwa hajambo. Walimuonyesha kitanda cha kulala katikati ya wagonjwa wawili, mmoja aliyelala fofofo kama maiti, wa pili alionekana akitapatapa kama mtu aliyekaribia kukata roho.
Waridi alilala kitandani hapo kwa dakika tano tu. Alikuwa akiwaza kwa makini. Hakuona anachofanya hapo hospitali. Wala hakuona sababu ya kuendelea kusubiri hadi atokee yule mtu ambaye aliamini angemwua na kushindwa kutimiza jukumu alilotumwa kulifanya. Wazo hilo likamfanya Waridi aamue kutoroka mara moja hospitalini hapo mara moja. Bila kufikiri mara ya pili aliinuka na kutoka kama anaelekea msalaani huku akipitia kanga moja ya yle mgonjwa aliyelala fofofo, akayafunika mavazi ya hospitali aliyovishwa na wauguzi ili ajisitiri. Alipotoka nje, akajitanda kanga hiyo na kufuata njia ya kutokea. Alijiingiza kwenye kundi la watu wengine waliokuwa wakitoka hospitalini hapo. Hakuna aliyemshuku kwa lolote. Dhamira yake ilikuwa kwenda Mburahati, akachukue chochote alichonacho, na senti kadhaa alizoficha chini ya godoro, kisha atoweke Dar na kwenda kokote mbali iwezekanavyo ambako mkono wa Prosper... usingemfikia kwa urahisi.
Lakini hakwenda zaidi ya hatua nne nje ya geti kabla ya kuisikia sauti ya mtu ikimwita kutoka nyuma. Akageuka kwa mshituko na kukutana ana kwa ana na Proper, ambaye alimjia akimchekea huku akisema kwa sauti ya dhihaka.
"Msichana mzuri... Umefanya vizuri... Nilitaka nije nikutoe mimi mwenyewe lakini kumbe umewahi kutoka. Pole kwa yote yaliyokukuta, ok usijali twende zetu, gari ile pale..."
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Kesho yake ilikuwa asubuhi yenye mawingu kiasu cha kuvunja nguvu ya jua kali ambalo lilikuwa likitishia kutawala. Mmoja kati ya wale askari waliomchukua Waridi pale baa alikuwa tayari kawasili kazini kwake. Mkuu wake wa kazi alihitaji ripoti kamili ya "Kushambuliwa kwa yule msichana malaya" Akamtaka pia kujitahidi waliotenda tukio hilo watafutwe na kupatikaba haraka iwezekanavyo kwani mchezo wao wa kubaka wasichana si mzuri kimaadili hususan mchezo wa hatari.
Askari huyo akalazimika kumsubiri mwenzake kwa muda mrefu, hakutokea. Ikamshangaza. Kwa kuwa makazi yake hayakuwa mbali na kituo cha polisi cha Magomeni, askari huyo aliamua kumfuata nyumbani, Alimkuta! Lakini alimkuta katika hali ambayo haikuwa ya kawaida, Kwani haikuwa jambo la kawaida mtu aanze kuvaa suruali kabla haijafunika matako, aache kazi hiyo ba kuanza kuinamia sakafu hadi kichwa kigonge chini mfano wa mtu anayeswali. Na zaidi ya hayo mgeni aingie baada ya kupiga hodi mara kadhaa bila kuitikiwa, lakini akukute ukiendelea kuinama kimya kimya. Dakika mbili, tatu hadi tano.
"Bobi", askari huyo alimwita mwenzake kwa mshangao, akijiuliza huu ni mzaha wa aina gani, na umeanza lini! "Bobi", aliita tena askari huyo huku akimtazama tena kwa makini zaidi askari huyo. Ndipo alipoanza kuona povu lenye damu damu likimdondoka mwenzake mdomoni na puani. Akaruka nyuma, kisha akakusanya nguvu na kumsogelea ili amchunguze vizuri zaidi. Akayaona macho yake yalivyoduaa, akauona ulimi ulivyotoka na kutembea nje ya meno, akaona... Hofu ikamkumbuka ghafla. alikuwa akitazama maiti ya askari mwenzake. Hima akarudi kituo cha polisi kutoa taarifa.
Marehemu alipelekwa hosptali ambako daktari hakuchelewa kutoa taarifa kuhusu ugonjwa uliosababisha kifo hicho. "Ugonjwa wa moyo", daktari alidai. Kwamba alikutwa na ugonjwa huo ghafla wakati akivaa nguo zake, ikabainishwa kuwa kifo cha askari huyo kilitokana na shinikizo la damu.
Hakuna aliyeshuku kuwa asakri huyo amekufa kwa sumu ile, ya aina yake, ambayo aliigusa kutoka kwa Waridi, na kuifikisha sehemu iliyokusudiwa kufika, mwilini mwake, bila askari huyo kujua.
Sumu hiyo iliandawaliwa kwa ajili ya Joram Kiango peke yake
Wakati huo huo Joram Kiango alikuwa akipokea simu iliyopigwa ofisini mwake.
"Sauti yako i tamu mno masikioni sister, yaelekea nawe u kiumbe mzuri sana. Siwezi kuukataa kamwe mwaliko wa mtu mwenye sauti nzuri kama hiyo, Baada ya saa moja nadhani nitafika... Haya... Ahsante... Umesema wapi vile... Heh... Light Lodge?... Hapo siyo?. Nitafika baada ya saa moja...", akaweka simu chini na kuukunja uso wake akimtazama Neema Iddy, katibu wake ambaye pia alikuwa akumtazama.
"Nani?", Neema alihoji kwa shauku.
"Anajiita waridi".
"Waridi? Anataka nini?" Joram alipochelewa kujibu. Neema aliongeza. "Sikujua Joram kama nawe u mroho wa wanawake kiasi hicho. Sauti tu unaridhika na kuahidi kumfuata? Angalia Joram. Utaingia katika mtego. Una maadui wengi katika nchi hii".
"Nalijua hilo", Joram alisema. "Siendi kwa sababu ya sura wala sauti yake kama nilivyosema. Kilichonivutia ni maelezo yake. Anasema yeye ni yule msichana ambaye alipigwa pale baa ya Forest of Flowers. Anadai kuwa nia yake ni kunishukru pamoja na kunipa habari fulani ambayo inasisimua".
"Malaya kama yule! Hana habari yoyote. Anachotaka ni kukupata wewe tu".
"Hapana", Joram alimkatisha. Sauti yake ndiyo iliyonifanya nivutiwe hata kumwahidi kuwa nitakwenda. Inavyoonyesha kuna kitu zaidi ya anachosema. Nahitaji kujua ni nini. Zaidi ya sauti, nadhani utakumbuka kuwa jana binti huyo alilia sana akilitaja jina langu. Sijui alivyonijua".
"Ni mimi niliyekutaja kwanza".
"Ni kweli, lakini hiyo siyo sababu ya kumfanya aniite jina langu mara nyigi tena kwa ufasaha kiasi kile. Ni kama mtu aliyekuwa akinifahamu kitambo".
"Wewe si mtu unayefafamika Joram?".
"Pamoja na hilo", Joram aliongeza. "Ni wapi alikopata namba yangu ya simu? Tuseme kwenye vitabu vya simu. Kwa nini ahangaike kiasi hicho? Na kwa nini iwe mapema hivyo? Neema, huoni ni mwujiza huu? Jana tu alikuwa hoi. Leo anazungumza kwa uchangamfu kabisa na yuko logi badala ya hospitali! Huoni kama kuna jambo hapo? Yaonyesha kuwa ananitafuta. Yawezekana hata jana alikuwa akinihitaji mimi tu hakuwa majeruhi wala mgonjwa!" Akasita kidogo kabla hajaongeza kwa sauti ya chini akisema: Na atanipata. Kwa muda mrefu nimekuwa sina kazi ya kufanya".
Wakati huo Joram alikuwa wima akivuta droo hii na ile, akiweka hiki mifukoni na hiki kiunoni. Mara akaanza hatua za haraka kuelekea mlangoni.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Yaani unakwenda Joram, mara hii!", Neema aliuliza kwa mshangao.
"Naam".
"Mapema namna hiyo? Si umemwambia baada ya saa moja?".
"Niliamua kumdanganya. Siamini kama yeye ananieleza ukweli mtupu, hivyo nami sioni ubaya wa kumweleza uongo kidogo. Nataka kufika mapema kidogo nione anachofanya".
"Lakini ujihadhari", Neema alimwambia wakati akivuka kizingiti cha mlango.
"Usijali Neema", Joram akamjibu bila kugeuka nyuma.
"Anakuja! Na atakufa!" Proper alimwambia Waridi.
"Ondoa hiyo mikunjo ya hofu usoni uvae suruali yako nzuri kama ilivyo. Akifika mpe tabasamu, mpe mapenzi, kisha mkaribibishe pombe. Usisahau chupa hilo hapo ni kwa ajii yake, akionja tu yamekwisha, asipoinywa mpake hii kwa hila".
Walikuwa katika chumba fulani, ghorofa fulani, katika jumba hili la light ambalo liko katika mtaa wa Lumumba, jijini Dar es Salaam. Proper alikodi chumba hiki kwa ajili ya kazi hii tangu jana alipomtoa Waridi kule hospitali. Usiku mzima aliutmia kumtisha Waridi kwa kila namna pale alipojaribu kuleta ubishi. Kisha alikuwa amemlazimisha kufanya naye mapenzi kwa njia zake za kinyama. Ilipofika alfajiri ndipo wakaanza kupanga mikakati ya mauaji.
Waridi alivishwa vazi jeupe la hariri, vazi hili lilifichua kila kitu kilichofaa kifichwa katika mwili wake. Kila jicho liliweza kuona mwili mzuri wa msichana huyo, ulikuwa ukimelelemeta kwa wekundu ndani ya mavazi hayo. Uso wake pia ulikuwa "kioo" kwa uzuri wake wa asili ulioshinikizwa kwa vipodozi murua vilivyotumiwa kistaarabu. Nywele zake zilitengenezwa kwa ile mitindo ya kisasa. Kwa kila hali, msichana huyu alionekana mtu tofauti kabisa na yule binti ambaye usiku wa jana tu alilala chini pale baa akiwa nusu uchi, akilia. Huyu alikuwa katika hali ambayo ilikusudiwa na ilitosha kuushinda ukaidi wa Joram Kiango dhidi ya wasichana warembo.
"Uwe msichana hodari. Ni kazi ndogo tu. Baada ya hapo utakuwa huru. Nitakulipa pesa za kutosha ukanisubiri Nairobi. Kutoka hapo tutakwenda zetu London au New York, tukatumie. Unasemaje?".
Waridi hakujibu.
"Mbona husemi neno?" Proper alimwuliza Waridi. "Hofu ya nini? Hii ni kazi ndogo mno kuliko ile uliyoifanya kwa Bomba. Na bado itakulipa pesa nyingi zaidi ya ule uchafu uliochukua. Jitie furaha na ucheke kidogo".
Kikcheko kilikuwa mbali na Waridi. Aliendelea kuduaa kama mzoga akisubiri lolote aliloelekezwa kulifanya. Hilo likamchukiza sana Proper.
Akasema. "Sikia wewe, endapo utavuruga tena mpango huu, sitasita kukuua papa hapa. Sasa hivi bado dakika ishirini Joram ataingia hapa. Nitakuwa chumba cha pili nikiangalia kila kitu. Ukishindwa au kuvuruga mpango huu nitakuua wewe na huyo Joram papa hapa. Nitakuua wewe kwanza na kisha Joram kwa hili hapa", akatoa bastola ndogo kutoka kwenye mfuko wa koti lake.
"Sipendi kukuua", Proper aliongeza. "Lakini ukinilazimisha nitaitumia kuwaua". Akaitazama tena saa yake. "JOram anaweza kuwa anakuja sasa. Natoka. Kumbuka kuwa niko karibu na tayari kukuua endapo utavuruga mpango huu. Sawa? Proper alitoka na kumwacha Waridi ameduwaa kama alivyokuwa.
Baada ya dakika kadhaa mlango wa chumba hiki uligogwa, kisha ukafunguliwa. Joram Kiango alichungulia ndani na kisha kuingia polepole macho yake yakiwa yamepumbazwa na uzuri wa Waridi. Hakutegemea.
"Sisiter... mimi ni mgeni wako nadhani. Naitwa Joram Kiango", alieleza Joram huku akiandaa tabasamu ambalo alijua linamfaa binti mzuri kama huyu.
Ndipo Waridi alipogeuka kumtazama.
Kama kuna wanawake ambao husimbua mioyo ya wanaume mara tu watokeapo mbele yao hata wanaume hao wakajisahau na kuzisahau shughuli zao, basi ni dhahiri pia wapo wanaume ambao huisumbua mioyo ya wanawake kwa kiwango kile kile. Na kama kweli wapo, miongoni mwao yumo Joram Kiango. Hayo yalijidhihirisha baada ya Waridi kumtia machoni Joram alipoingia chumbani.
Moyo wake ulipoteza mapigo kwa sekunde kadhaa. Roho yake ilihisi kupaa nje ya mwili wake. Kadhalika, damu ilimsisimka kiasi cha kumfanya ahisi ganzi mwili mzima. Hivyo, hakuweza kuyaondoa macho yake juu ya umbo la Joram ambaye alimsogelea polepole. Nusura wazimu umpande Waridi alipoona uso na tabasamu la Joram, lililotosha kuwa tiba kwa maradhi yake. Maradhi aliyoamini kuwa hayangeweza kutibika.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Kwa bahati mbaya, Waridi hakuwahi kupenda mwanaume katika maisha yake. Hivyo hakujua mapenzi ni nini. Hakuwahi kuyaonja. Kama angejua, angefahamu nini kitatokea. Badala yake alihisi maumivu moyoni na huzuni kubwa akilini mwake. Akanusurika kutokwa na machozi. Hakujua nini kinamtokea. Isipokuwa kitu kimoja tu alikifahamu, Joram hakuwa mtu wa kufa, Hakuona sababu ya kumwua, Asingeweza...
Tazama alivyosimama mbele yake kwa upendo na utulivu kama malaika asiye na hatia. Tazama anavyochekelea kwa furaha kama nuru, Mtazame. La, huyu kijana si mtu wa kufa. Waridi akawa ameamua hivyo.
"Nadhani mimi ni mgeni wako, mpenzi, Joram alisema tena, akinyoosha mkono wake kumgusa Waridi kwenye bega lake la kuume.
Joram alikuwa ameshangazwa na uzuri wa msicha huyu. Vipi wengine waumbwe kwa upendeleo kiasi hiki wakati wengine wasitofautiane sana na vinyago? alijiuliza. Mavazi mazuri ya msichana huyu pia yalimchanganya Joram; yalikuwa mavazi mapya ya thamani kubwa, kisha ya kihuni kama yalivyondaliwa mahususi kwa ajili ya kumtongoza! Hicho hakikumshangaza Joram, Lakini alishangazwa na uso mzuri wa msichana huyu ukiwa katika dimbwi la majonzi, mashaka, hofu na msiba. Hilo halikumshangaza hata kidogo.
"Ndio...ka... karibu kaka", waridi alianza kusema huku akibabaika,
Joram alimvuta mkono na kumwongoza hadi kitandani, ambako alimketisha kisha naye akaketi kando yake huku akiendelea kuushika mkono wa Waridi.
"Nilikwambia kuwa sauti yako ni tamu kama ilivyo sura yako? Naamini sikukosea. Ama kweli umeumbika bibie. Ulimhonga nini muumba hata akakupendelea?"
Sauti ya Joram, tabasamu lake likasindikiza kila neno, hali hiyo ikamfanya Waridi aanze kuchangamka. Akasahau yote yaliyokuwa mbele yake na kujikuta kazama katika maongezi na Joram. Katika kipindi hicho kifupi bila kujifahamu Waridi alijikuta tayari akiwa ameufunua moyo wake wote kwa Joram, akimsimulia matatizo yake yote. Alipotanabahi alikuwa akisema: "Najisikia kutoweka nje ya nchi hii".
"Kwanini?".
Swahili hilo lilimzindia Waridi. Hakujua yapi alikuwa tayari kuyatamka ambayo hayakustahili kuiacha milki ya kinywa chake, Hofu ikamrejea. Akalikumbua jukumu lililokuwa mbele yake: kumfanya kijana huyu kuwa marehemu. Ama ni yeye atajayefanywa marehemu.
Hofu hiyo, ilizidi baada ya Joram kuinuka na kuiendea meza iliyokuwa na chupa mbili za pombe huku akisema: "Bia hii? Unaonaje nikianza kuimimina tumboni mwangu ili kupoza joto la Dar es Salaam kabla hujanieleza sababu za kuniita hapa? Siamini kwama kweli umeniita kwa ajili ya kunishukuru tu, yaani hilo likusukume kunitafuta..."
"Usinywe hiyo pombe", Waridi alifoka.
"Kwanini mpenzi? Nilidhani umeiandaa kwa ajili yangu", Joram alifuatwa na tabasamu la kukata na shoka.
Waridi alikuwa akitetemeka. Lakini asingeweza kusahau maneno ya yule mtu katili Proper alipomwambia: "Nitakuwa chumba cha pili... Ukishindwa tena nitakuua papa hapa..." Waridi hakupenda kufa, lakini pia hakuwa tayari kumuona kijana huyu asiye na hatia, afe. Afanye nini? Kwa kutojua la kufanya akaanza kulia. Mikono ya Joram ilitua tena mabegani kwa Waridi akimfariji na kumkumbatia huku akisema.
"Kama hutaki ninywe hii bia ni wazi kwamba kuna zawadi kubwa na tamu zaidi ya bia uliyoiandaa kwa ajili yangu. Kwa bahati mbaya nina mazoea ya kunywa pombe kabla ya yote. Kwa maana hiyo niruhusu ninywe bia moja tafadhali".
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Usi..." Waridi alijaribu kufoka tena. Joram alimzuia kwa kuuziba mdomo wake kwa kiganja cha mkono wake huku akiweka kinywa chakr karibu na sikio la Waridi, akamnong'oneza.
ITAENDELEA
Simulizi : Salamu Kutoka Kuzimu
Sehemu Ya Pili (2)
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Najua kitakachotokea. Sinywi pombe hiyo. Acha nijifanye kama nakunywa ili nimpumbaze huyu anayetaka kuniua. Nitakuomba wewe uwe msiri wangu. Mwache aamini kuwa ameniua. Mwache kila mtu aamini kuwa nimekufa. Nataka kufahamu hawa waliokusudia kuniua jambo gani wanakusudia kutenda".
waridi aliduaa. "Ume... umewezaje kujua? aliuliza kwa kunong'ona.
"Niliwahi kufika eneo hili mapema na kumsikia alivyokuwa akikuamru. Nawe pia lazima ufahamu kuwa uko hatarini. Huyu ni mtu hatari. Mara tuu utakapotoka hapa, toroka uende kokote asikoweza kukufikia. Sasa acha nijifanye nainywa pombe yake". Joram akaongeza sauti kusema. "Glasi? Acha ninywe kihuni".
Joram aliifungua chumpa moja na kuingia nayo msalani ambako aliimimina nusu kwenye tundu la choo, Akarudi na kuitua mezani huku akiendelea kuongea na Warid, mazungumzo yao yalifanyika taratibu kwa sauti ya chini. Mara kadhaa Joram alimshika waridi na kumtomasa hapa na pale kwa ajili ya kumtoa hofu.
"sasa mpenzi sikia", aliongeza. "Ninaye mgeni ambaye atakuja ofisini kwangu baada ya nusu saa kuanzia sasa. Baada ya kumalizana na mgeni huyo, leo kutwa nzima nitakuwa huru. Waonaje niende ofisini mara moja na kurudi sasa hivi? Naamini leo tutashinda pamoja kwa furaha sana. Naamini itakuwa siku njema twetu".
"Sawa", Waridi alijikongoja kujibu.
"Tafadhali nikukute, ukiwa kama ulivyozaliwa. Ikiwezekana, kitandani, sawa?"
"Bila shaka".
Mara tu Joram alipotoweka machoni mwake, Waridi alijikuta akirejewa na hofu. Ile hakika na ushujaa ambao alikuwa ameuhisi kwa kusikia sauti ya Joram na kuyaona macho yake yang'aavyo sasa ilikuwa kama ndoto tu. Ndoto ya kale. Hakujua lipi afanye. Akaendelea kuduwaa kimya, akitazama huku na huku kama aliyetegemea kumwona Zibril akimjia kwa lengo ka kutwa roho yake.
Waridi angetimua mbio Proper alivyoingia ghafla huku akimtazama Waridi kwa macho ya kutisha. Waridi angeweza kukimbia kama ukuta usingekuwa umemtenga na dunia ya nje. Alichofanya ni kurudi nyuma hatua kadhaa hadi alipoegemea ukuta, macho yenye hofu kayatoa kama kondoo aliyekuwa juu ya madhabahu, akisubiri kutolewa kafara.
"Mwanakharamu... malaya mkubwa, mwana wa malaya mkubwa...", Proper alifoka. "Umekosa walau ushujaa wa kunidanganya kuwa hawara yako amekunywa pombe niliyomwandalia? Mara hii umesahau kuwa mmekubaliana naye adai kuwa ameinywa ili asingizie kuwa kafa. Nakusikitikia Bi. mdogo. Namsikitikia pia huyo hawara yako. Hajui afanyalo. Anadhani kuwa anacheza na watoto wadogo kama alivyozowea. Nilikuwa nimemfanyia hisani kubwa ili afe kistaarabu hakutaka. Kajitia ujanja. Sasa atakufa kifo cha kusikitisha zaidi".
Jodor Proper aligeuka kama anataka kutoka. Mara kama aliyekumbuka jambo alimgeukia tena Waridi na kusema. "Nawe malaya mwovu hufai kuishi zaidi. Huna faida duniani wala haki ya kuishi tena. Utamfuata mpenzi wako Bomba akhera. Mpe salamu zangu, mwambie hongera kwa hila zake zisizo na ila". Akageuka na kutoka.
Machozi yalikuwa yamenyauka machoni mwa Waridi. Sasa aliiona dunia kama kitu ambacho kilikuwa kando yake. Naam, maisha yake yalikuwa ukingoni. Asingeweza kutilia mashaka sauti ile ya Proper yenye uhakika. Sauti ambayo masikioni mwake ilikuwa kama saut ya mauti yenyewe.
Kwanini aendelee kusubiri? alijiuliza. Kwanini asubiri kifo cha mateso na kashfa? Akajiuliza kwanini asitangulie? Sasa macho yake yalikuwa yakitambaa kila mahali kutafuta silaha yoyote ambayo ingefaa kumtoa roho. Mara macho ya waridi yakatua kwenye ile chupa yenye pombe yenye sumu iliyoandaliwa kwa ajili ya Joram, bila kufikiri kwa mara ya pili aliiendea ile chupa yenye pombe akajimiminia tumboni mwake.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Mara Waridi akapata faraja kubwa ambayo ilimfanya asahau hofu na kudharau vitisho vyote vilivyokuwa mbele yake. Alijiona yu njiani hatua chache tu kufika katika milki mpya. Milki ambayo itampa uhuru kamili.
Furaha hiyo ikamuongoza Waridi, alitoka ndani ya chumba hicho na kuiendea lifti. Akatelemka hadi chini. Aliiacha hoteli na kuanza safari ya kuelekea kituo cha mabasi. Mavazi yake yakiwa kama yalivyokuwa, umbo lake likiwa kama lilivyo, na sura yake nzuri ikiwa imepambwa na tabasamu, viliyafanya macho ya wanaume kumtazama kwa mshangao wenye tamaa. Baadhi waliguna walipomuona, wawili walimkonyeza na mmoja alidiriki hata kumfuata. Wote walipata tuzo kwa tamaa zao. Tuzo ambalo lilikuwa tabasamu pana zaidi ambalo liliwafanya wabaki wameduwaa nyuma yake hoi bin taabani.
Waridi akaendelea na safari yake. Mwendo wake ukiwa nyongeza nyingine ya maneno kwa watazamaji. Akiwa kajaza nyuma, kakatika kati na kunyooka alivyonyokeana, ilikuwa kana kwamba hatembei bali anafanya maonyesho ya miondoko kama wanavyofanya warembo katika mashindano ya miss. Mwenyewe akiwa hana habari hizo, aliendelea na msafara wake hadi alipokifikia kituo na kujiunga na umati wa watu waliokuwa wakisubiri usafiri wa umma.
"Gari hii hapa dada", mtu mmoja alimwambia Waridi. Ilikuwa teksi. Waridi hakufanya hiana, akajitosa ndani ya teksi hiyo huku akisema. "Nipeleke Mburahati",
"Vizuri, lakini waonaje kama tukipitia hapa Embassy Hoteli tukapate walau bia mbili mbili baridi?", dereva alitupa ndoano yake.
"Samahani, leo nina haraka, nitafute siku nyingine".
"Kesho".
"Sawa..." waridi alilaghai. Rohoni akiamini kuwa kesho hatakuwa Dar es Salaam. Hatakuwepo hapa nchini, wala popote Afrika. Atakuwa nje. Nje ya dunia. Aliendelea kuwaza kwa furaha huku akimwitikia dereva huyo, "Ndio", kwa kila dereva huyo alilosema wakati hata hamsikii. Walipofika mbele yavijumba vayo, Waridi alimtaka dereva asimame. "Ni hapa, asante kaka", dereva hakuyaamini masikio yake, "Yaani uaishi hapa. Katika vijumba hivi? Na unaishi hapa dada?", dereva alishawishika kuuliza.
"Hapa ndio kwangu", Waridi alijibu wakati akitelemka kutoka ndani ya gari.
"Hapa?", dereva aliuliza tena kwa mshangao. Hakutia neno lingine. Badala yake aligeuza gari lake na kurudi alikotoka kwa mwendo wa kasi.
Walidi akapokelewa na wenzake waliojawa na mshangao. "Iwe", alisema mmoja wao. "Ulikuwa wapi".
"Na ilitokea nini hata ukaondoka bila kuaga?", alihiji mwingine. Maswali yalikuwa mengi mno. Waridi hakuwa na muda wa kuyajibu yote. Wala hakukumbuka ajibu maswali gani. Alichokumbuka ni jinsi alivyoingia chumbani kwake na kujilaza kitandani akisubiri kifo. Usingizi mzito ukamchukua.
Alipoamka ilikuwa usiku wa saa tatu. Chumba cha pili kitanda cha mwenzake kilikuwa kikilalamika kwa uzito wa viumbe waliokuwa wakikitumia. Naye alikuwa akigongewa mlango. Mteja akainuka na kumwendea. Alikuwa mtu mwenye umbo la mwili wa mtoto na uso wa mzee. Alikuwa na pesa zake mkononi tayari. "Leo sifanyi kazi", Waridi alimwambia mteja huyo na kufunga mlango wake. Hakujali malalamiko ya mteja huyo. Alikuja mwingine. Na mwingine tena. Wote Waridi aliwakatalia. Nao wakaondoka shingo upande.
Halafu akaja huyu mteja ambaye hakukubali kuondoka. Alikuwa kavaa kofia kubwa iliyofunika uso wake na koti kubwa lililofunika hadi miguuni. Aliingia kwa kujlazimisha na kufunga mlango nyuma yake huku akisema, "Lazima".
"Leo sitaki".
"Hata kwa bei kubwa?".
"Hata ukitoa milioni".
Mtu huyo alicheka kidogo. "Mimi wanitaka. Umekuwa ukinisumbua muda wote huu", Alitupa koti lake chini na kubaki katika suruali na shati. Akaivua kofia yake na kuitupa juu ya koti. Ni hapo Waridi alipomtambua. Macho yenye hofu kubwa yakamtoka.
"Bila shaka utakuwa umenikumbuka ", alisema polepole. "Unadhani nilikusudia ufe kistaarabu kwa ile sumu?, Ile ilikuwa maalumu kwa ajili ya Joram Kiango peke yake. Wewe ni mwovu mwenye dhambi nyingi. Unastahili kufa kishenzi".
Kabla Waridi hajafahamu kama ilimpasa kufanya nini, alijikuta tayari kadakwa ghafla kwa mkono kwa mkono wenye nguvu, ambao uliibana mikono yake yote miwili. Haraka kamba zikapita mikononi mwake. Alipotanabahi kupiga kelele, alijikuta katupiwa dude fulani kinywani ambalo lilimziba kinywa. Mara akatupwa chini na kudungwa sindano ambayo ilimlegeza hata asiweze kutapatapa.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Kisha kisu kikali kilichomolewa kutoka ubavuni na kuanza kupita juu ya mwili wake. Maumivu yalikuwa makali ajabu, lakini hakuwa na uwezo wa kulalamika. Alichoweza kufanya ni kuendeleo kukodoa macho yenye dalili zote za hofu na maumivu. Macho hayo yalishuhudia mikono yake ikikatwa mmoja baada ya mwingine na kuwekwa juu ya kitanda. Kisha tumbo la waridi likafumuliwa na utumbo kumiminika katika sinia lililokuwa mezani. Baada ya sekunde kadhaa alikuwa tayari amekata roho pindi kichwa chake kilipokatwa na kuwekwa juu ya debe, kando ya kitanda.
Baada ya kuridhika na kazi yake. Proper alizivua nguo zake zenye damu na kuzifunika katika mifuko ya koti lake ambalo alilivaa na kisha kutoroka zake nje polepole kama wateja wengine. Hapo nje aliwakuta wateja kadhaa ambao walisimama kwa namna ya mstari wakisubiri zamu zao. Akafanya haraka kuiendea sehemu aliyoficha gari yake.
Mteja aliyeingia baada ya Proper aliduwaa kwa kutokumuona Waridi. Kisha alishangaa kuiona mikono ya mwanamke huyo iliyolala peke yake juu ya kitanda. Halafu akakiona kichwa kilicholowa damu, kimelala chali. Hakuyaamini macho yake. Na ilipomtokea kuamini alihisi akili yake ikipaa. Alipiga kelele kwa nguvu na kuanza mbio akielekea barabarani, Alianguuka, akainuka na kuendelea kukimbia.
Mtewa mwingine alichungulia tu na kugeuka akianza safari ya kurudi zake alikotoka kimya kimya.
Ni mteja wa tatu aliyetoa taarifa kwa majirani na wenzake kuhusu kilichomtokea Waridi. Yeye pia alitoweka. Majirani walichanganyikiwa kwa muda mrefu. Mmoja wao alitapika. Wawili wakalia kwa nguvu. Umati mkubwa wa watu ulifika. Polisi pia hawakuchelewa.
"Umesema u nani wewe?".
"Naitwa Joram Kiango".
Inspekta Mkwaju Kombora hakuyaamini masikio yake. Jina la Joram Kiango lilikuwa maarufu kichwani mwake kama mbwa anavyoifahamu harufu ya chui. Mzee huyu alimfahamu vyema Joram. Yule kijana machachari aliyefanya mengi dhidi ya wahujumu uchumi na majasusi hatari ambao jeshi la polisi lilielekea kukata tamaa. Yule kijana nadhifu sana, mpole sana, mwenye nguvu na akili. Si huyu mzee aliyesimama mbele yake katika vazi la Kiarabu, akiwa amevaa kanzu nyeupe, kapiga kilemba, mwenye ndevu nyingi, uso uliofunikwa na miwani na mkononi kashika fimbo ambayo ilimsaidia katika mwendo wake wenye dalili zote za udhaifu wa kizee,
"Joram?", Inspekta Kombora akauliza tena.
"Naona huniamini kwa vile hujanifahamu Inspekita", ilisema sauti ambayo Kombora alielekea kuifahamu kwa mbali,lakini sura haikuwa ya Joram.
"Pengine niondoe miwani na haya madevu ya bandia ili uweze kunitambua". Madevu yakatolewa na miwani ikavuliwa, Uso ulisimama mbele yake ukitabasamu, Alikuwa ni Joram Kiango halisi ambaye Inspekta Kombora alimfahamu vyema.
"Nini sasa unafanya Joram?", alishangaa Inspekta Kombora. "Mchezo huu una lengo gani?".
"Siyo mchezo inspekta. Niko kazini. Unionavyo hapa mimi ni marehemu. wapo watu wameniua. Nataka niendelee kuwa marehemu ili...
Inspekta Kombora alimkatisha na kumwekea mkono begani huku akisema, "Sikia Joram. Kama ni mzaha subiri nitakapokuwa huru ndipo utakapoufanya tena mchezo wako, tucheke pamoja. Kwa sasa niko katika mkasa mzito ambao unaweza kuhatarisha usalama wa jiji endapo mtu huyo mwenye roho ya kinyama hatapatikana".
Habari hiyo ikamvutia Joram. "Mtu gani?", Joram alihoji mara moja.
"Hujasikia tu? Nadhani wewe hupitwi na neno".
"Kusikia?".
"Kuhusu msichana huyo aliyeuawa kikatili kuliko ilivyowahi kutokea. Polisi wamefanya kuokota viungo vyake kimoja baada ya kingine ndipo ukapatikana mwili mzima wa marehemu. Mtu aliyefanya mauaji hayo ni mnyama zaidi ya wanyama wengine wa kawaida. Mtu mwenye kumchinja msichana mrembo kama yule".
"Sijakupata Inspekta, yaani..." kisha Joram akapunguza kasi kuhoji kuhusu tukio hilo kwa kituo. Inspekta Kombora akamweleza yote kuhusu tukio zima lilivyotokea usiku huo huko Mburahati.
Hakukuwa na sababun za kuupeleka mwili huo hospitali", Inspekta Kombora aliongeza. "Viongo vyote vya marehemu vimeletwa hapa katika chumba cha maabara. Kama utapenda kutazama vitu vya kutisha unaweza kwenda maabara, inatisha sana".
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Nitapenda kumwona tafadhali".
Inspeta Kombora akaiacha ofisi yake na kumuongoza Joram kuelekea maabara ambako alifungua friji na kutoa kichwa cha msichana mrembo. Joram alikitambua kichwa hicho kuwa cha Waridi. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake, alihisi machozi yakimdondoka. Aliyafukuza macho hayo kwa tabasamu huku akinong'ona kama mtu anayesali. "Ni Waridi! Mungu akurehemu. Naamini ni mapenzi yako kwangu ambayo yamekufanya ustahili adhabu hiyo ya kinyama. Naahidi nitakulipia kisasi".
Sala hiyo ilimfikia Inspekta Kombora. Akamgeukia Joram kwa mshangao na kusema, "Kumbe unamfahamu msichana huyu? Tafadhali turejee ofisini ili unisimulie kuhusu mkasa mzima ulivyotokea".
"Sijawa na cha kusimulia", Joram alijitetea. Hata hivyo alilazimika kusimsimulia Inspekta Kombora yote aliyoyajua. Alieleza jinsi alipomwona Waridi kwa mara ya kwanza pale baa akiwa ametegwa kwa sumu iliyokusudiwa kumwua yeye. Akaeleza pia yaliyotokea katika chumba ambacho waridi aliandaliwa kwa sumu ile ile ili amnyweshe Joram kwa hila. Ambacho Joram hakueleza ni jinsi alipofika hapo kabla ya wakati na kubahatisha, ingawa kwa taabu, kumwona mwuaji yule akitoa maelezo kwa Waridi. Hilo aliliacha ili apambane nalo binafsi. Hakupenda kuwaachia polisi ambao aliamini wangeweza kuharibu mapngo wake wa kumtia mikononi mwuaji.
"Ina maana binti huyu marehemu ndiye yule msichana aliyetoroka hospitali baada ya kuokotwa kando ya baa", Joram akatikisa kichwa kukubaliana na swali la Inspekta Kombora.
"Ndiye. Basi anastahili kifo cha aina hiyo. Kwa nini hakutoa taarifa polisi, tungeweza kumsaidia. Alishirikiana na wahalifu kuandaa njama za kufanya uhalifu".
"Inawezekana au isiwezekane", Joram alijibu kwa mkato. "Aweza kuwa alilazimika au kulazimishwa. La muhimu sasa ni kumpata huyo mwuaji".
"Ndio... apatikane haraka. Wewe humjui?".
Joram alikanusha. "Angalia bwana mdogo. Ninavyookufahamu mimi bila shaka wajua mwengi zaidi ya haya uliyonieleza. Nawe kama uonavyo hawa ni watu hatari kuliko unavyofikiri. Usiwachukulie mzaha, Ucheze nao kama ilivyo kawaida yako".
"Kawaida yangu sina mzaha wa mwuaji Inspekta", Joram alijibu. "Tena naamini kuwa nitawafikisha mikononi mwako mapema zaidi. Ninayo nafasi nzuri sana. Sasa hivi wao wanadhani kuwa nilikunywa ile dawa na sasa niko mahututi au marehemu tayari. Imani hiyo itawafanya wapate jeuri ya kuendelea na mipango yao kama walivyokusudia. Nataja kujua lengo lao, wanakusudia kufanya nini, na watu hawa ni akina nani, baada ya kufahamu hivyo nitawaleta mikononi mwako.
"Kazi hiyo ndiyo iliyonifanya nijibadili kuwa katika hali hii Inspekta. Nimeona nitoweke machoni mwao. Kusudi langu kwako ni kukuomba uitangazie dunia kuwa nimefariki ghafla. Nadhani watafurahi na kuendeleza mipango yao. Ndipo nitakapofufuka na kuwashangaza kwa kuwatia mikononi.
Walijadiliana kwa muda ofisini. Kombora akawa ameafikiana kwa taabu sana na Joram. Nia ya Joram ilikuwa awaachie polisi kufanya kazi yao kwa makini. Lakini maelezo ya Joram yalimtua Inspekta Kombora hata akakubali japo kwa shingo upande. "Kumbuka ninavunja sheria zote za kushiriki katika uongo mkubwa kama huu. Hivyo. usiniangushe kwa kushindwa kutimiza ahadi yako ya kuwatia watu hawa mikononi mwa sheria", Inspekta Kombora alimwambia Joram.
"Wanifahamu vizuri Inspekta. nakuhakikishia kuwa Siwezi kushindwa kamwe", Joram alimjibu akiweka vyema ndevu zake za bandia na kuvaa miwani yake. Akautwaa mkongojo wake na kuiacha ofisi ya Inspekta Kombora kwa mwendo ambao ulimfanya Inspekta huyo ambaye hucheka kwa nadra sana aangue kicheko kipana.
Usiku huo taarifa ya habari ya Radio Tanzania Dar es Salaam ilibeba habari ambazo ziliwashitua wasikilizaji wengi kote nchini.
"...Joram Kiango yule mpelelezi mashuhuri wa kujitegemea amefariki ghafla akiwa nyumbani kwake kwa maladhi ambayo bado hayajathibitishwa. Madaktari wanaendelea na uchunguzi watatoa taarifa za kifo hicho hivi karibuni baada ya uchunguzi,,,"
Haikuwa habari njema hata kidogo. Wala hakuna aliyetarajia kuisikia. Kila aliyemfahamu Joram alitegemea kuwa kijana huyo angeuawa au kufa kwa risasi au madhara mengine kutoka kwa adui zake. Kufa kwa maradhi! haiwezekani!.
Taarifa za habari za sauti ya Kenya na Ujerumani ziliidaka habari hiyo haraka na kuitagaza kwa mapana zaidi... "Yule kijana machachari"... Walisema wakenya, "The Iron boy..." walimwita hivyo wajerumani... "Amefariki leo ghafla. Yawezekana na njama za wahujumu ambao walimuogopa sana kijana huyu kama moto".
Ndipo watu walipolazimika kuamini. Wengi walisikitishwa na kifo hiki. Wengine walitoa machozi. lakini Wachache walishangilia.
Nyumba hii iliyobomolewa kwa bomu ilikuwa katika mtaa wa Manda Magomeni Mikumi. Ilikuwa nyumba ambayo kwa muda mrefu haikutumiwa kutokana na kutokamilika kwake tu. Joram alikuwa ameichagua nyumba hii kwa ajili ya kujificha baada ya kuitazama mara kwa mara kila alipopita katika mtaa huu na kuona ilivyokaa vizuri kwa siri. Ilikuwa imezungukwa na kichaka cha miti ambayo awali ilikusudiwa kuwa bustani. Haikuwa rahisi kwa mtu wa nyumba jirani kufahamu yanayotokea katika nyumba hii kwa jinsi zilivyotengana.
Zaidi, ilikuwa na njia nyingine ya uwani ambayo ilipitia katika uchochoro hadi mitaa ya nje kabisa. Kuhamia hapa ilikuwa siri yake binafsi ingawa Inspekta Kombara alimsihi sana amfahamishe wapi amejificha, Alikuwa amehamia hapa usiku wa manane baada ya kujipitishapitisha ili kuhakikisha kuwa hafuatwi au kuonekana na mtu. Mzigo wake pekee ulikuwa ni Suitcase yake ambayo ilichukuwa vifaa vyake muhimu ikiwa pamoja na silaha ndogo,CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Usiku huo wa kwanza alilala vyema. Alfajiri aliamka na kujiandaa kwa kuvua ujana na kuvaa uzee. Baada ya kukamilisha taratibu za uzee alilificha vizuri begi lake na kutoka hadi polisi ambako alikamilisha mipango yake na kurejea mafichoni akisubiri muda alioupanga ili aanze harakati zake.
Joram alikuwa na hakika kuwa kazi hii isingemchukua muda kuimaliza. Jambo lililomtia matumaini ni kule kujua kuwa adui zake walikuwa wakisubiri kifo chake ili waanze shughuli zao. Kadharika, mmoja kati ya adui hawa hakuwa mgeni kwake. Alichungulia alipokuwa akitoa amri kwa marehemu Waridi na kuipata picha yake. Insingemchukua muda mrefu kumfahamu kikailifu.
Kitu kimoja Joram hakujua. Hakujua kuwa makazi haya ya siri aiyohamia hayakuwa yake binafsi. Yalikuwa malazi ya Luta Magambe, mmoja kati ya mamia ya vijana wazurulao katika Jiji la Dar es Salaam. Luta alikuwa ameingia Jijini miaka zaidi ya kumi iliyopita, akitokea kwao kijijini katika moja wapo ya Wilaya za mkoa wa Kagera. Alikuja Dar es Salaam kwa nia njema ya kutafuta kazi baada ya elimu yake ya msingi. Jiji likamlaki kijeuri kama linavyowalaki wote. Kazi haikupatikana kwani hakuwa na mtu wa kumfanyia "mpango" wala pesa za "motisha".
Akaambulia kuangukia katika vibarua vya kutwa. Pesa alizopata zikawa ndogo mno kulingana na mahitaji ya Jiji. Kila siku akawa mtu wa "Kuchacha". Hilo likamtuma kutumia muda wake wa ziada kuwachomolea wasafiri wa Uda na Daladala. Tabia hiyo haikuchelewa kumfikisha Keko akiwa na majeraha mengi usoni. Alipotoka Keko hakuwa luta mwenye nia njema tena, bali mtu ambaye yuko tayari kufanya lolote mradi apate chochote.
Msimamo huo mpya ulimanya apoteze chumba na kukosa marafiki wa haja. Rafiki zake pekee walikuwa wahuni wenzake na walikutania "kazini". Baada ya "kazi' kila mmoja alijua lake.
Siku alizopata, alistarehe kwa kulewa, kujipatia wasichana wazuri na kulala vizuri katika majumba ya wageni ama kwenye nyumba za wasichana hao. Alipokosa alijutia na kujisahaurisha kwa kuvuta bhandi na kujilaza katika jumba hilo bovu.
Hivyo kwenye alfajiri hiyo aliona kama mwujiza kuona 'mzee' huyu mwenye dalili ya pesa na sura ya Kialhaji akitokea ndani ya moja ya vyumba vya jumba hili akiitumia njia yake ya siri! Mara moja wazo likamjia Luta?. Kwamba mzee huyu alikuja katika ghofu hili kwa sababu maalumu. Sababu ambayo Luta aliamini kuwa haikuwa nyingine zadi ya kuficha pesa au vitu vya thamani, Wazo hilo likamtuma kuanza upekuzi akitafuta chochote ambacho mzee huyo alikificha. Hakupata kitu. Hata hivyo alikuwa bado akiendelea na upekuzi wake 'mzee' aliporejea. Hima akajipenyeza katika chumba cha pili ambamo alijificha vizuri. Joram hakumuona. Darubini ya adui yake Joram kutoka nyumba ya pili pia haikuweza kumuona. Alitulia akimchungulia Joram ambaye aliketi akifanya mambo yake.
Kisha Bagambe alimuona mtu mwigine akinyatia nyumba hii mkononi kashika vitu ambavyo alivificha kwa hadhari chini ya mlango, Baada ya mtu huyo kushika hapa na pale aliondoka eneo hilo kwa hadhari na ukimya ule ule.
Kitu gani kitatokea?, Bagambe alijiuliza, Hakika moja alikuwa nayo. kuwa hii ilikuwa nafasi yake pekee ya 'kuukata'. Kwamba leo lazima ungekuwa mwisho wake wa maisha ya kubahatisha na mwanzo wa maisha mapya. Ingekuwaje vngine na eti bahati zinamfuata hadi huku badala ya yeye kuzifuata kwenye vituo vya basi? Hakuona sababu ya kuendelea kusubiri.
Kwa hadhari mfano wa paka anayemnyemelea panya, aliiendea sehemu hiyo aliyoona kitu kikifichwa. alipofika alipekua taratibu. Kisha aligusa waya fulani ambao hakutarajia kuuona hapo. Aliutazama waya huo kwa mshangao. Mshangao ambao ulikatizwa na mlipuko mkali uliomfanya apae juu na kutua chini akiwa tayari ametawanyika vipande mfano wa nyama za kopo, zinazoandaliwa kwa ajili ya kusindikwa.
****************************
Mlipiko huo ulimkuta Joram Kiango akiwa amesimama wima, fimbo mkononi. Aliduwaa alipoona ghafla mtu akizuka mbele yake na kupaa angani ambako alitawanyika vipande vipande. Lakini hakupata muda wa kuendelea kuduwaa, kwani wakati huo huo kila kitu kilikuwa kikipaa na kutua huku na huko kwa kishindo cha kutisha.
Kila kitu pamoja na Joram mwenyewe. Alijikuta angani kisha akajibwaga chini akifuatwa na lundo kubwa la vitu vizito ambavyo vilimfunika juu.
Joram hakuwa na muda wa kusikia maumivu pia. Alihisi kama mtu aliyepoteza kichwa au ubongo. Fahamu zikamtoka na nafsi yake kuchukuliwa na kiza kinachotisha.
******************************
Kifo cha kusikitisha! Joram aliwaza hivyo, karibu kila mtu kati ya umati mkubwa uliosimama kando kuizingira nyumba hiyo. Macho yenye hofu na huzuni yalikuwa yakiwatazama askari ambao walikuwa wakiviokota viungo vya marehemu kimoja baada ya kingine na kuvitia katika sanduku. Ni watu wachache sana walioweza kutazama tukio hili kwa muda mrefu. Wengi walitupa jicho kwa sekunde kadhaa na kisha kugeuza nyuso zao upande mwingine huku wakiguna na kufuta machozi. Mama mmoja alisikika akilia kwa sauti.
Ilikuwa mara ya kwanza kwa wengi wao kushuhudia tukio la mtu aliyepoteza maisha kwa njia hii ya kutisha.
Miongoni mwa walioshuhudia tukio hilo alikuwwepo Jodor Proper. Alikuwa mmoja wa watu waliofika mapema katika eneo hilo. Lakini alimkuta mtu wake aliyetega bomu hilo akijifuta vumbi baada ya ule mweleka alioupata kutokana na tofali lililomponda kichwani. Yeye alikuwa mmoja kati ya 'wapita njia' wanne waliojeruhiwa katika ajali hii. Proper alimsaidia mtu huyu kama asiyemfahamu. Walipopata mwanya walinong'onezana: "Kazi nzuri sana, Sasa nenda zako..."
Mtu huyo alipoondoka. Proper aliendelea kutazama 'ajali' huku akijitia kunung'unika. Lakini ndani ya moyo wake alikuwa akisherehekea na kushangilia sana tukio hilo. 'Kifo kinachomstahili kabisa' Aliwaza kwa furaha. "Mnofu mmoja mmoja! Na ajiunge basi tuuone huo ushujaa wake".
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Wazo la kwamba huenda huyu akawa si adui yake mkubwa Joram Kiango halikumjia akilini. Ingawa haikuwa njia rahisi ya kuthibitisha mabaki hayo ya marehemu, lakini katika uchunguzi wake Proper alifanikiwa kuiona ile fimbo ya Joram na madevu yake ya bandia ambayo yaliokotwa na askari mmoja na kumwonyesha Inspekta wao ambaye alibabaika kama mtu aliyeguswa na simba. Kitendo hicho kilimfanya Proper ajisikie kucheka huku akijituliza. Wangetangaza nini tena wakati dunia nzima imefahamishwa zamani kuwa Joram Kiago amefariki dunia?.
Proper alipotoka katika eneo hilo kwa tabasamu, alikuwa na wazo moja tu la kuendelea na mipango yao bila kuwa na hofu yoyote. Kikwazo pekee alichoogopa yaani Joram Kiango kilikuwa tayari kimeingia kuzimu, kikiwasalimia babu zake huko.
Mmoja wa maofisa wa polisi alipendekeza wafanye uchunguzi wa kina ili kuhakiki kama eneo hili lilikuwa na maiti ama mareruhi wengine zaidi waliokandamizwa na kifusi. Lakini majirani wa eneo hilo waliwahakikishia polisi kuwa nyumba hiyo haikuwa na watu. Wakaondoka haraka haraka kwani kazi ya kufukua vifudi ilikuwa nzito, ambayo hakika ingewatoa jasho. Wakaondoka na mwili wa marehemu wakiuacha umati wa watu ukiendelea kufika katika eneo hilo kutazama kilichotokea.
Usiku ulipoingia, giza liliwaondoa watu katika eneo hilo likabaki katika hali yake ya kawaida.
Unono, huyu alikuwa mwanamke wa makamo, mfupi kiasi, mnene wa kutosha, mweusi kupindukia, mama huyu alikuwa mmoja kati ya watu wengi walioshuhudia ajali hii ya mtu kuuawa kwa bomu. Mama huyu alikuwa miongoni mwa umati huo, kama wananchi wengine alisema hili na kusikiliza lile, macho yake yakifanya kazi ya kutazama kwa hofu tukio hilo pamoja na polisi kadhaa, ambao walikuwa katika pilika pilika za kukusanya mabaki ya marehemu huyo.
Kichwani Unono alikuwa na mawazo tofauti, nje kabisa ya tukio la msiba huo uliotokea eneo hilo. Alikuwa na mawazo mchanganyiko wa matatizo ya kiuchumi na mapenzi. Mama huyu alihisi kuwa sehemu hiyo ingeweza kumfanya apate ufumbuzi wa tatizo lake moja ama yote mawili yanayomtatiza.
"Usiku..." aliwaza moyoni mwake.
Kimaumbile, Unono hakuwa na umbo la kuridhisha wala hakuwahi kujidanganya kuwa ana sura nzuri. Ukweli huo alikuwa ameubaini tangu enzi za usichana wake alipojiona akikua miongoni mwa vijana wa kiume ambao walionekana kumwepuka kama jini na kumtazama kama jinamizi. Wakati huo huo aliambulia kuwaona wenzake wakifuatwa na vijana wa kiume na kubembelezwa kama malaika, wakipewa lugha tamu na matendo ya kimapenzi. Ndipo alipoanza kujitathimini katika kioo.
Akagundua kuwa pamoja na kuwa na sura mbaya, Alitisha na kuchukiza kwa jinsi alivyojengeka kama kilema ingawa hakuwa na kasoro yoyote kimaumbile. Hivyo maisha yake yaliyofuata aliishi akifahamu kabisa kuwa tunu ya kuzaliwa mwanamke yeye isingemsaidia kama wanawake wengine. Aliamini kuwa katika maisha yake lazima atoe jasho ili aweze kuishi.
Jasho lake alilitoa kwenye vilabu akiwauzia wanywaji makongoro ya ng'ombe ambayo aliyanunua machinjioni na kuyachemsha kwa maji na chumvi. Sura yake haikumtendea wema katika biashara yake. Mwanamke huyo aliyekuwa na tama zote za kike, alipata mume wa kufariji kwa kwa bahati. Na alipompata, ilikuwa mhali mwanaume huyo kumrudia. Naye Unono hilo halikumshangaza kamwe kwani hilo lilikuwa jambo la kawaida katika maisha yake. Hayo yalimtokea kwa nadra sana. Hivyo siku nyingi Unono alikuwa mhitaji. Ndipo akabuni mbinu za kutembea sehemu fulani fulani usiku, sehemu ambazo alikuwa na matumaoni ya kukutana na wanaume ambao nafsi na hali zisingewaruhusu kuchunguza. Walevi wachelewao kurejea majumbani kwao usiku, wazururaji wasio na makazi maalumu, na walinzi wanaokesha wakilinda nje usiku, hawa ni miongoni mwa wateja ambao Unono aliwahi kuwapata ili kutimiza haja zake. Baadhi waliwahi hata kumpatia pesa.
Kwa hivyo Unono akakusudia kujaribu bahati yake kwenye eneo hili lililolipuliwa na bomu. Hangekosa kufua dafu pale. Askari mmoja ama wawili wasingekosa kuwekwa hapa kwa ajili ya kulinda mazingira. mmoja wao asingekosa kumtupia maneno iwapo angecheza vema karata yake. Na hata wawe wote wawili angebabaishwa na nini angestahimili. Eti kakosa mapenzi ya mume kwa muda mrefu sasa. Ni mawazo hayo yaliyomfanya Unono afunge biashara mapema na kurejea nyumbani. Aliogaa, akajipaka mafuta yake yenye harufu nzuri, mafuta ambayo aliyanunua kwa shingo upande. Alivaa baibui lake jeusi bila vazi lingine lolote mwilini.
Alijikuta akiingiwa na wasiwasi. Alikuwa peke yake, katikati ya kiza katika eneo ambalo mchana huo lilikuwa la maafa. Akawaza kurudi, lakini alijikongoja hadi alipofika kando ya vifusi vya jumba hilo. Alitupa macho kila upande, hakuonana dalili yoyote ya mlinzi. Baada ya mizunguko kadhaa, aliamini kuwa sehemu hiyo haikuwa ikilindwa. Akasononeka moyoni.
Mara likamjia wazo jingine. Yawezekana katika jumba hili mlikuwa na vitu vya thamani ambavyo angevichukua na kuviuza! Wazo hili likamtuma Unono kuanza kuchungulia, akashika kile na kujipenyeza pale. Alipata mwanya ambao ulimwingiza ndani ya kifusi hicho. Mikono yake iliendelea kupeleleza kwa makini, macho yakifanya juhudi kutazama.
Ghafla Unono aligusa kitu ambacho kilimshitua. Kitu chenye dalili ya uhai. Nyoka? alijiuliza baada ya kuutoa haraka mkono wake. Baada ya kutulia kwa makini, aligundua kuwa alichogusa ni mwili wa binadamu. Ugunduzi wake ulimshitua zaidi. Maiti nyingine! aliwaza akiinuka na kuanza kuondoka.
Kisha ushujaa ukamwingia na kumfanya ahairishe safari yake na kuuinamia mwili huo kwa uchunguzi zaidi.
Inspekta Kombora alikuwa mgonjwa mahututi, ingawa hakuwa tayari kumweleza daktari wake kuhusu kuumwa kwake wala hakutaka kujieleza mwenyewe ni maradhi gani yanamsumbua. Alijiona tu yu hoi bin taaban, hali ambayo ilimtokea ghafla baada ya kuviona vile vipande vya mwili wa binadamu vilivyotawanywa kwa bomu. Lakini kilichomuuguza zaidi ni kuokotwa zile ndevu za bandia alizokuwa amevaa Joram Kiango.
Joram kafa! lilikuwa wazo lililomtesa zaidi ya ukweli Inspekta Kombora. Joram ambaye jina lake lilikuwa tishio kwa waovu wote wenye nia mbaya kwa nchi na wananchi wake! Joram ambaye alikubali kuiweka roho yake hatarini mara kwa mara kwa lengo la kuwakabiri maadui wenye nguvu na uwezo wa kutisha! Joram, kijana mwenye moyo wa jiwe na mwili wa chuma! Joram amekufa?...
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Miaka mingi ilikuwa imepita, kiasi kwamba Inspekta Kombora hakumbuki siku gani aliyotokwa na machozi. Leo hii, akiwa peke yake ofidini, akiitazama meza yake, alihisi chozi likipenya kwenye vipingamizi vyote na kuelea juu ya mashavu yake, jambo ambalo lilimshangaza zaidi. Mshangao ambao ulimezwa na hasira kali za ghafla. Akaupiga mkono wake mezani kwa nguvu nyingi na kuvifanya vifaa kadhaa vilivyokuwa mezani hapo vidondoke sakafuni. Hakujishughulisha kuviokota.
"Joeam kafa!... aliendelea kuwaza kwa machungu.
Mara swali la kutisha likamjia akilini, Ataitangazia nini dunia iliyoamini kuwa Joram alikufa siku nyingi, atasema nini badala ya ule uongo wa kifo kilichosababishwa na sumu. Dunia ingemwelewa vipi mzee huyu mwenye dhamana kubwa serikalini.
Halafu akajikuta akitetemeka ghafla lilipomjia swali la kutisha zaidi. Nani hawa wauaji na wanakusudia kufanya nini? Kwamba, hawa si adui wa mzaha, Hakuwa na shaka na swali lake hilo. Yeyote aliyehusika kumwua Joram na hasa aliyemwua kikatili kiasi kile, hawezi kuwa mtu wa mzaha hata chembe. Wala hakuwa mtu anayecheza isipokuwa aliyedhamiria kufanya jambo baya mno ambalo hakutaka Joram Kiango aliingilie kama walivyofanya majuzi kwa kuwavunja uti wa mgongo wale waroho waliokuwa katika hatua za mwisho za kupindua nchi na kuiuza kwa mabepari. Hawa ambao wameshawishika kumwua Joram kwa bei yoyote ile wanakusudia kufanya nini?.
Ilimuumiza zaidi kujiona yeye kama mkuu wa usalama akae kimya wakati akijua kuwa kuna uovu uliojificha kando ukinyemelea, wakati huo huo akiwa hajui ni uovu gani na utatokea upande gani. Alikuwa amekwisha fanya mengi. Tangu jana wakati akitazama mabaki ya marehemu wakati yakikusanywa, alikwisha chukua hatua zote za upelelezi dhidi ya mauaji hayo. Kikosi cha askari kilikwisha teuliwa kitambo, kikifuatilia kila kichochoro ambacho kingeweza kuwafikisha mbele ya adui, Maswali mengi pia yalikuwa yakiulizwa. Lakini yawezekana kabisa maswali hayo yangeweza kuulizwa kwa miaka bila majibu kupatikana. Mtu pekee ambaye ama alikuwa na jibu tayari, ama angeweza kulipata mapema zaidi, sasa alikuwa marehemu.
Hata hivyo afanye nini? Aendelee kusubiri mtu au watu hawa wafanye yote waliyokusudia wakati yeye akiendelea kustarehe juu ya kiti hiki kama Ofisa wa Polisi alijiuliza. Afanye nini kuongeza nguvu ya mkono kuwatafuta maadui hao? Nani anaweza kuwa na walau fununu ya kinachotokea?.
Ni katika kujiuliza maswali hayo alipomkumbuka Katibu Mahsusi ya Joram Kiango, yule msichana mzuri, Neema Iddy. Akajilaumu kwa uamzi wake wa kumpinga msaidizi wake mmoja ambaye alipendekeza Neema aletwe ili amthibitishie marehemu.
"Ataonyeshwa nini? Huone kama tunaweza kumpata msichana wa watu ndoto za kutisha katika maisha yake yote au hata wazimu kwa kumuonyesha haya mabaki ya mtu aliyekuwa mwenzi na mpenzi wake?". Kombora alikuwa amemjibu hivyo askari huyo. "Hapana", aliongeza. "Mwacheni".
Zaidi ya hayo, nadhani mnakumbuka kuwa hii ni siri ya watu wachache sana, watakaowajibika kufahamu aliyefariki ni Joram Kiango. Wengine wote lazima waendelee kuamini kuwa alifariki ghafla kabla ya kifo hiki.
"Sasa aliuona umuhimu mkubwa wa kumuona Neema. Hivyo bila ya kuaga wapi aendako, alipanda gari na kuielekeza iliko ofisi ya Joram.
Aliikuta ofisi hii imefungwa. Akajielekeza Temeke, ambako alifahamu jina, mtaa na namba ya nyumba ya Neema.
******************************
Ilikuwa siku ndefu kwa Neema Iddy. Ingawa kila siku ni kama siku nyingine lakini siku hii aliiona hivyo kutokana na ile harara kubwa iliyomkaria rohoni ikimtia shauku ya kumwona Joram Kiango na kutaka kufahamu hicho alichokuwa akikishughulikia safari hii, hata akaweza kujibadili na kuwa mkongwe kiasi kile, na kutangazwa uongo kuwa amekufa. Neema alihisi kuwa mkasa huu bila shaka ni wa kutisha na wa hatari kuliko yote iliyotangulia, au sivyo, Joram asingechukua hashari kiasi kile, wala polisi wasingeafiki kutangaza uongo. Ilimsikitisha Neema alipomkumbuka Joram alivyomnyima siri hiyo kwa madai ya kwamba, ni "Hatari" kumhusisha.
Siku ya jana nzima, Neema alikuwa ameshinda katika hali hiyo. Akihesabu dakika na masaa, akisubiri wakati ambao ingetanagzwa upya redioni: "Joram yu hai... Na amesababisha kukamatwa kwa wahujumu ambao..." Ni hapo alipokuwa akiishia Neema. Na ni swali hilo ambalo lilikuwa likimweka roho juu. Hamu ya kujua safari hii adui ni nani na walikusudia kufanya nini.
Neema alitabasamu, akakumbuka sifa ambayo Joram aliipata kwa kusuluhisha mambo magumu magumu. Mara hii, akawaza atailetea nchi yake gani? Wazo kuwa angetokea mtu, amshinde Joram, hasa baada ya kutangazwa kuwa amekufa, kama walivyotaka wao, swali hili halikuwa na nafasi katika fikra za Neema. Akawa mtu ambaye anasikia sifa za wapelelezi hodari duniani, pamoja na kusoma hadithi za kubuni juu ya upelelezi, Bado Neema alikuwa hakumbuki kama alikwisha tokea yeyote mwingine ambaye alikuwa na mtindo wa aina ya Joram Kiango. Mtu asiyeogopa wala kutishiwa, mtu asiyekata tamaa, mtu anayejua kila anachofanya! Neema alihisi furaha na faraja kubwa kuona kuwa yeye ni msichana pekee ambaye amepata fursa ya kushirikiana na mtu huyu shujaa. Hadhi iliyoje!.
Ni mawazo hayo yaliyokuwa yakimfanya Neema atabasamu. Lakini alihitahidi kuificha tabasamu hilo kwa huzuni ya uongo kila alipotokea mtu wa kumpa pole kwa kifo cha 'mwajiri' wake. Ilikuwa ni wajibu wake kujifanya yumo katika msiba.
"AMekufa kijana yule mzuri? Siamini" angesema kijana mmoja. Neema bila ya kumtazama ya kumtazama usoni angemjibu kwa masikitiko.
"Amekufa... ndiyo hali ya dunia.
Kifo cha ghafla! Wamempa sumu.
"Haijajulikana".
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Ama kweli ndege mjanja hunasa kwenye tundu bovu".
Angeondoka huyo, aje mwingine. Kila mmoja alisema hili au lile.
Neema aliwasikiliza wote na kuwafanya waondoke wakiwa wameamini kile ambacho hawakutaka kukiamini, kuwa Joram Kiango amefariki.
Neema akiwa katika hali hiyo, tabasamu rohoni, huzuni moyoni, alisikia gari likisimama mlangoni mwao na baadaye mlango wa chumba chake ukagongwa. Aliingia Inspekta Mkwaju Kombora.
Macho ya Inspekta Kombora yalimfanya Neema ahisi jambo mara moja kuwa hakukuwa na habari njema. Neema akiwa si mgeni kwa Inspekta Kombora baada ya kuzungumza naye mara kwa mara kuhusu harakati na mipango ya Joram, Neema alimjua Inspekta huyu vizuri, alifahamu wakati gani yuko katika hali mbaya kimawazo na wakati gani anajisingizia hali mbaya. Leo ilikuwa dhahiri kuwa kuna kitu kikubwa kimemkaria rohoni.
"Kuna nini Inspekta?", Neema alihoji baada ya kumaribisha kiti.
"Joram amekufa!" Inspekta Kombora alimwambia.
"Najua", Neema alijibu kwa tabasamu.
"Nadhani bado hujanielewa. A-me-ku-fa", alisisitiza,
Kidogo Neema akashangaa. "Ndiyo mzee! Nadhani hata wewe unajua. Imebidi ujifanye hivyo kwa ajili ya watu hawa ambao wanamtafuta Joram. Muda si mrefu atafufuka na jambo ambalo naamini litakusisimua Inspekta".
Kombora akamkatisha kwa kumweleza kuhusu tukio zima la bomu lililosababisha kutawanyika kwa viungo vya marehemu. "Nimeona nitakutia katika msiba na simanzi iwapo nitakuonyesha mabaki hayo ya Joram. Ama kweli kilikuwa kifo cha kusikitisha sana dada yangu. Sikuona kama ungestahili kumwona mtu uliyempenda sana akiwa katika hali kama ile".
Ndipo Neema alipopata ukweli wa mambo ulivyo. Aliduwaa kwa muda, Macho kayatoa akimtazama Kombora wakati hamuoni. Neema alihisi damu yake imesimama kabisa na fikra kukwama. Joram kufa! Fahamu zilipomrejea, alinong'ona maneno fulani ambayo Kombora hakuyasikia. Kisha akaondoka mbio hadi chumbani kwake. Alifunua mto na kutoa bastola yake ndogo aliyozawadiwa na Joram katika moja ya sherehe zake za kuzaliwa. Akaishika imara na kuitingisha huku akipiga kelele: "Nitamwua yeyote aliyekuua Joram..." alifoka Neema, lakini sauti ilitoka ikinong'ona hata isiyafikie masikio yake mwenyewe. Alipokumbuka kuwa alikuwa hamjui mwuaji huyo, aliirejesha silaha hiy katika maficho yake ya siri na kubaki ameduwaa katikati ya chumba chake. Kisha akarejea ukumbini na kuketi chini.
"Samahani Inspekta", Neema alisema polepole, "Kwa muda mrefu sijapata habari mbaya ya kuumiza kama hii",
"Si habari ya kupendeza hata kidogo. Mimi pia imenitia homa. Pole sana".
Baada ya kutafakari kwa muda, Inspekta Kombora akayarejesha maongezi yake kikazi. Alimsihi Neema kumweleza chochote anachofahamu ambacho kingeweza kupatikana kwa mwuaji au wauaji hao mapema iwezekanavyo. Hata hivyo Inspekta Kombora alivunjika moyo baada ya kugundua kuwa Neema hajui lolote la maana. Hivyo akaondoka kimya kimya kurejea ofisini kwake baada ya kumkumbusha Neema kuwa kifo cha Joram kiendelee kuaminika kuwa alifariki ghafla kwa maradhi ambayo hayajafahamika.
Neema alibaki katika hali ile ile ya butwaa, moyo ukiwa kama uliokufa ganzi na ubongo kudumaa. Alihisi kama mtu aliyefika ukingoni katika safari yake ya maisha. Kwake Joram alikuwa kila kitu. Alikuwa furaha na faraja katika maisha yake, heri na neema yake. Hakuona vipi angeweza kuyahimili maisha bila tabasam la Koram mbele yake. Hakujua vipi ataweza kusisimukwa bila harakati za Joram dhidi ya adui zake.
Mapenzi ya Neema na Joram hayakuwa yale ya kimwili kati ya msichana na mvulana. Lakini Neema aliyaona kuwa ni makubwa zaidi ya uhusiano wa aina hiyo. Makubwa yaliyojengeka katika misingi mikubwa zaidi. Ni kweli kuwa zipo nyakati ambazo Neema alijikuta akimhitaji Joram kimwili kwa tamaa kali kuliko alivyowahi kuhitaji kitu chochote. Siku kama hizo alikesha kitandani akisali kuomba Joram atokee, amkumbatie. Ni kweli pia kuwa kuna siku ambazo aliwahi kuona tamaa hiyo ikiwaka katika macho ya Joram kwa nguvu kiasi kwamba ilitokea kama mwujiza alipofaulu kutotamka kile ambacho alitamani kukitamka. Kitu ambacho jibu la Neema lisingekuwa zaidi. "Sawa tu".
Wote walifanikiwa kuzitawala nafsi zao. Kama alivyowahi kusema Joram: "Akili isipoutawala mwili ni sawa na gari kuacha barabara na matokeo yake hakuna asiyefahamu", Joram! ambaye sasa ni marehemu!
Bado haikukubalika kichwani mwa Neema kuwa Joram amekufa. Ilimrudia akilini siku ile ambayo alimwona Joram kwa mara ya kwanza.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Wakati huo Neema akiwa mwandishi wa habari katika gazeti moja hapa nchini. Siku hiyo alipata barua kutoka kwa mtu asiyejulikana, ikimdokeza kuwa mtu mmoja mkubwa serikalini alikuwa amehusishwa katika mauaji ya watu watatu ambao maitiza zao ziliokotwa huko Manzese. Habari hii ilikuwa imeishitua sana nchi. Neema akiwa mwandishi anayependa kuripoti habari kubwa kama hii, aliamua kwenda kutafuta ukweli na kuandika habari hii kwa undani ili kuligusa kila jicho la msomaji.
Ilibidi Neema ajifanye kuwa mwanamke kahaba ili aweze kuingia ndani ya jumba la kigogo huyo. Huko ndani Neema alifanya kila mbinu hadi kuteka mawazo ya mtumishi wa mkubwa huyo wa serikali, ambaye bila kufahamu aliweza kueleza habari zote za siri zinazofanywa na kigogo huyo. Neema alipofanikiwa kuujua udani wa mauaji hayo alitumia mlango wa uwani kutoka katika jumba hilo na kurejea ofisini kuwahi nafasi katika gazeti la kesho. Lakini hakuweza kufika mbali baada ya kujikuta akiwa katikati ya watu wanne wenye bastola ambao walimpiga na kitako kichwani Neema akapoteza fahamu. Fahamu zilipomrejea alijikuta yuko baharini, katika jahazi, mmoja wa majambazi hao akiwa amemshika kichwani na mwingine miguuni wakijiandaa wakijiandaa kumtosa majini. Alilia kwa nguvu zake zote lakini majambazi hayakuonyesha dalili yoyote ya kumuonea huruma. Mmoja wao alikuwa akisema kwa kebehi.
"Kamlilie mama aliyekuzaa na hao bwana zako waliokutuma kuchunguza mambo yasiyokuhusu".
"Sikieni, mimi si mpelelezi..." alijaribu kusema. hakuna aliyemsikia. Wakamwinua juu na kumchezesha bembea ili wamtupe kwa urahisi. Neema alikoma kulia. Badala yake akayafumba macho yake akisubiri kifo. Ni hapo lilipotokea jambo ambalo hakuna aliyelitegemea. Mtu aliibuka ghafla kutoka mahali fulani katika jahazi hilo na kuwashambulia watu hao kwa mtindo wa upiganaji ambao Neema aliwahi kuuona katika michezo ya sinema tu. Dakika chache baadaye maadui wote walikuwa wamelala chini wakigalagala kwa maumivu. Mtu huyo alimwunua Neema na kuanza kumkumbatia huku akimtazama kwa tabasamu.
"Pole sana mpenzi", alitamka mtu huyo baada ya kuona mshangao hauyaachi macho ya Neema.
"Umeyaokoa maisha yangu... Asante sana", Neema alisema kwa sauti ya unyenyekevu. "U nani wewe?".
"Naitwa Joram Kiango".
"Joram!", Neema alifoka kwa mshangao. Alikuwa amepata kusikia jina jilo likihusishwa sana katika kuwakabiri majambazi, wahaini na wahalifu wengine. Alikuwa amelisoma mara kadhaa magazetini. Lakini hakupata kumtia machoni. Ndio kwanza akaona hawakukosea sana wale walioandika kuwa yu kijana mzuri. Walichosahau ni kutoweka neno 'sana' katika sifa zake. Kwa keli Neema hakutegemea kama mtu mwenye tabia zile za kupambana na maadui wengi ana kwa ana bila hofu angeweza kuwa hivi; mzuri sana, mtaratibu sana, macho yenye upole, sauti... "Joram Kiango!" akaita tena. "Umeniokoa lakini sijui namna ya kukushukuru".
"Huna haja", Joram alimjibu. "Ni mimi mwenye haki ya kukushukuru. Siku zote nilimshuku mkubwa yule kuhusika katika yale mauaji lakini sikuwa na ushahidi wa kutosha. Wewe umefanya kazi nzuri Neema. Umeniwezesha kupata ushahidi mzuri. Hawa wauaji watasema ukweli watakapofika mahakamani..."
"Ni wewe uliyeandika ile barua?", Neema aliropoka ghafla.
"Ndio", Joram alijibu baada ya kutabasamu. Nadhani utaniwia radhi kwa kukufanya chambo. Nilikufahamu siku nyingi na kujua kuwa u msichana shujaa. Nilijua kuwa ungefanya vizuri, na umefanya vizuri... vitu vyote viwili ambavyo nilivihitaji unavyo, ushujaa na uzuri..."
Neema alijikuta akimkumbatia Joram. Walitulia kwa muda na tena kwa faraja. walipoachana Joram aliiwasha mashine ya jahazi na kuiendesha hadi pwani ya bahari ambapo aliwakabidhi majambazi hao kwa polisi. Siku chache baadaye mahakama ilitoa adhabu kali kwa 'mkubwa' huyo kitanzi na majamazi kufungwa kifungo cha maisha jela. Neema alipotoka mahakamani alimsaka Joram bila mafanikio. Ilikuwa baada ya wiki kadhaa walipokutana bila kutegemea. Hawakutengana tena.
Na sasa Joram amekufa, Neema aliwaza. "Yeyote aliyemwua nitahakikisha anamfuata", Neema alifoka kimya kimya. "Naapa".
Usiku ulipoingia ulimkuta Neema akiwa bado kaduwaa pale pale alipokuwa. Alikuwa hajatia chochote mdomoni ingawa jirani zake walimfuata mara kadhaa wakimshawishi kula. Aliinuka na kuwasha taa ya umeme. Wakati wa kulala ulipowadia, alijilaza kitandani kama kawaida na kuyafumba macho yake, lakini usingizi haukumjia. Hadi asubuhi alikuwa hajatongoa walao lepe.
Kisha mlango uligongwa na kufunguliwa polepole. Neema alikuwa amesahau kuufunga kutokana na kuzongwa na mawazo. Aliyeingia ni mtu ambaye Neema hakupata kumwona katika maisha yake yote. Mtu huyu aliyarejesha mawazo ya Neema katika ulimwengu wa kawaida, Dunia ya mtu kushutuka, kushangaa, kucheka na kukasirika. Mtu huyu angeweza kumfanya yeyote amtazamaye afanye lolote kati ya hayo. Lakini Neema alishangaa tu.
Hiyo ilitokana na umbo la mtu huyo. Neema alifahamu kuwa yu mwanamke kutokana na mavazi na matiti yake manene, ambayo badala ya kukaa kama ilivyo kawaida ya matiti katika kifua cha mwanamke haya yalikuwa kama matuta yaliyolimwa shambani pasi na mpangilio maalumu. Sura yake haikuwa na chochote kinachofaa kuitwa 'uzuri' Macho yake hayakupendeza kutazamwa! Pua lake! Midomo!... Neema akajikuta anatokwa na mshangao na kujikuta akiingiwa na mshituko. "Mwenzetu huyu kweli aliumbika", Neema akajisemea.CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
"Naitwa Unono", mgeni alianza kujieleza akisimama kando ya kitanda. Hakujishughulisha kujaribu kutabasamu. Wala Neema hakuona kitu kinachoitwa tabasamu kiliwahi kuupitia uso huo, Wala hakuona kama tabasamu lingewezekana kwa hali ipi. "Wewe ndiye Neema Iddy?", aliuliza.
"Ndiyo", Neema alijibu.
"Unamfahamu Joram Kiango?".
Neema alibadilika na kuonekana mnyonge zaidi. "Wewe ni nani?", Neema akahoji. Unono hakujishughulisha kujibu. Badala yake akasukuma swali lingine.
"Unajua kuwa Joram amekufa?".
"Na... Najua. Wewe ni nani? Neema aliendelea kuhoji.
"Huna haja ya kunifahamu. Naona dhahiri kuwa u mpenzi wake. Au siyo?" Neema alipochelewa kujibu Unono akaendelea, "Unampenda kweli?"
Mbali na ubaya wa sauti ya mwanamke huyu, na ubaya wa macho yake. Neema aliona kitu kingine pia. Naam, aliona wivu. Naam, mkabala wa mwanamke huyu ulionyesha hisia fulani, wivu. Mwanamke huyu wa ajabu anamwonea wivu kwa Joram Kiango.
|Ni mpenzi wangu", Neema akajikuta akifoka. "Ndiyo nampenda. Hata kwa kifo chake nitaendelea kumpenda. Wewe u nani na unahusika vipi baina yangu na mwandani wangu?".
Unono hakujibu upesi. Aliutia mkono kifuani mwake na kuutoa ukiwa umeshika picha ndogo. "Kama kweli unampenda. Kama kweli utaendelea kumpenda, jitahidi umjue huyu ni nani, na anaishi wapi ili leo jioni nikija hapa uniambie wapi anapatikana".
"Umepata wapi picha hii?" Neema aliuliza baada ya kuipokea na kuitazama kidogo, "Na picha hii inahusikaje na kifo cha Joram?".
"Inahusika... Niliipata kwenye mifuko ya marehemu dakika chache baada ya kifo chake . Naamini mwenye picha hii anahusika. Pata maelezo kamili ya picha hiyo. Nikirudi hapa nitakueleza nini zaidi cha kufanya. "Baada ya maelezo hayo Unono aligeuka na kuanza kuondoka zake kwa mwendo wa kuchekesha.
Neema aliitazama tena picha hiyo. Ilikuwa sura ya mwanaume mwenye dalili ya heri kimaisha na kimadaraka. Lakini picha hii ilionekana kama muhusika hakujiandaa kupigwa picha hiyo. Ilikuwa sura ambayo haikuonekana ngeni sana machoni mwa Neema. "Huyu anahusika vipi na kifo cha Joram?", Neema alijiuliza. Na mwanamke yule, Unono analijua asemalo? Akajiuliza kwanza amewezaje kumpata yeye (Neema) kirahisi hivyo katika jiji kubwa kama hili? Lazima kuna jambo hapa. Mawazo haya yakamfanya Neema aamue kufuata maelekezo ya Unono. Kwa kuwa alikuwa bado msichana tena aliyepitia taaluma ya uandishi wa habari, alifahamu wapi angeweza kupata habari za mtu huyu.
Muda mfupi baadaye Neema alikuwa njiani akielekea kituo cha mabasi. Alipanda UDA ambalo lilimfikisha mjini, Akatelemka na kuiendea ofisi yake ya awali, katika shirika moja la habari. Baada ya kupewa pole nyingi na rafiki zake kufuatia kifo cha Joram, aliomba ruhusa ya kutumia maktaba ya picha. Humo alitafuta picha ambayo inafanana na ile aliyokuwa nayo mikononi. Hakuipata, Alipokaribia kukata tamaa akawauliza wengine kijanja kama wanamfahamu mtu huyo.
Mtu wa kwanza kuitazama picha hiyo alicheka na kisha kumtazama Neema kwa mshangao. "Umeipata wapi picha hii Neema?".
"Unamfahamu?", Neema aliuliza kwa msisitizo akiwa na matumaini.
"Wewe Neema, yaani humfahamu huyu?" Alijibiwa kwa swali lingine. "Huyu siyo Profesa Kimara? Karibu kila mtu anamfahamu".
"Kimara yupi?".
"Chain Kimara. Yule Profesa ambaye anaandika kitabu juu ya uwezekano kuifanya mimea aina ya wanga inayolimwa hapa nchini iweze kukua na kukomaa haraka katika kipindi cha nusu ya muda wake wa kawaida. Huwa anakuja hapa ofisini mara kwa mara kueleza jinsi anavyoendelea na utafiti wake",
Ilikuwa habari njema kwa Neema, Anapatikana wapi?", aliuliza Neema.
"Nani anajua?" alijibiwa. Kwani unamhitaji kwa ajili gani Neema?"
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Neema alijitahidi kumlaghai alivyoweza. Kisha akachukua kitabu cha orodha za simu na kulitafuta jina la Profesa Kimara. Haikumchukua muda kulipata, Anuani ilionyesha kuwa anapatikana katika mtaa wa India katika nyumba za msajili wa majumba namba 107. Taarifa hizo Neema akazinakiri nyuma ya picha hiyo na kisha kuanza safari ya kutoka akimshukuru mkutubi. Moyoni Neema alijaa furaha. Ilikuwa rahisi kuliko alivyotegemea.
ITAENDELEA
0 Comments:
Post a Comment